Utamwambia Nini Mwislamu?
1 Je, umewahi kumhubiria Mwislamu? Kama umewahi, labda ulijua kwamba Waislamu wanaitikadi kwa bidii katika Mungu. Hata hivyo, hawajui mengi juu ya Paradiso inayokuja duniani kama ilivyotabiriwa na manabii wa Yehova, nasi tungependa kushiriki nao tumaini hilo. (1 Tim. 2:3, 4) Habari ifuatayo yapaswa kukusaidia utoe ushahidi wa kutosha.
2 Waislamu huamini Allah, au Mungu, nao huamini kwamba Muhammad ni nabii wa Mungu. Kitabu chao kitakatifu ni Kurani, na dini yao yaitwa Uislamu, unaomaanisha “unyenyekeo.” Kurani husema kwamba kudanganya na ibada ya sanamu ni makosa, kwamba Mungu ni mmoja, na kwamba yeye si sehemu ya Utatu. Pia, hufundisha kutokufa kwa nafsi, moto wa mateso, na paradiso ya kimbingu. Waislamu hukubali kwamba Biblia ni Neno la Mungu lakini wao huamini kwamba imebadilishwa, ilhali Kurani, ikiwa ingali katika lugha yake ya awali, haijafisidiwa.
3 Uwe Mwenye Urafiki, Mwenye Busara, na Mwenye Utambuzi: Unapomhusisha Mwislamu katika mazungumzo, uwe mwenye urafiki na mwenye busara. (Mit. 25:15) Kumbuka kwamba itikadi za Waislamu zimefanywa imara sana na kwamba wamejifunza baadhi ya hizo kwa moyo. Hivyo, kusababu juu ya mafundisho ya kidini na kujithibitishia wenyewe mapenzi ya Mungu ni nini, hakujawa sehemu ya ukuzi wao wa kiroho. (Rom. 12:2) Ili kusaidia Waislamu, subira na uelewevu ni sifa za maana.—1 Kor. 9: 19-23.
4 Epuka kutumia misemo ambayo kulingana na Mwislamu atakushirikisha na mtu wa Jumuiya ya Wakristo. Julisha wazi kwamba wewe si Mkatoliki wala Mprotestanti, kwamba wewe ni tofauti. Iite Biblia Kitabu cha Mungu. Kwa kuwa Waislamu wanachukia sana msemo “Mwana wa Mungu,” mara nyingi inafaa kutoutumia au kuzungumzia jambo hilo mpaka maendeleo ya kiroho yatakapofanywa. Hata hivyo, unaweza kusema juu ya Yesu, ukimrejezea kuwa nabii au mjumbe. Epuka kubishana. Ukiona kwamba hasira yaanza kupanda, ondoka kwa upole mara moja.
5 Inafaa zaidi kuongea na mtu mmoja tu wala si na kikundi. Mara nyingi, inapendekezwa wanawake kutoa ushahidi kwa wanawake, na wanaume kwa wanaume. Bila shaka, si lazima iwe hivyo sikuzote, lakini wapaswa kuamua vizuri. Pia, Waislamu wengi huwa na hisi nyepesi kuhusu yale wanayoona kuwa mavazi na mapambo ya wanawake yasiyo ya kiasi. Akina dada wanahitaji kujua jambo hilo.—1 Kor. 10:31-33.
6 Mambo ya Kuzungumzia: Sema waziwazi kuhusu ukuu wa Mungu na upendo wake. Usisite-site kusema kwamba wewe ni mwamini wa kweli, kwamba Mungu ni mmoja (si Utatu), na kwamba ibada ya sanamu ni kosa. Zungumza juu ya uovu ulimwenguni leo—vita, msukosuko wa raia, chuki ya jamii, na unafiki ulio wazi miongoni mwa watu wengi wa kidini.
7 Broshua The Guidance of God—Our Way to Paradise itakupatia ufahamu wenye kina wa habari za kuzungumzia ambazo zaweza kutumiwa kuanzisha mazungumzo na Waislamu. Imekusudiwa kuvutia Waislamu ambao huishi katika mazingira ambayo huenda wakahisi huru kujifunza Biblia.
8 Waweza kutumia utoaji huu:
◼ “Nafanya jitihada za pekee kuongea na Waislamu. Nimekuwa nikisoma juu ya dini yako nami naamini nasema kweli kwamba Waislamu huamini Mungu mmoja na manabii wote. [Ruhusu jibu.] Ningependa kuongea nawe kuhusu nabii wa kale aliyetabiri kugeuzwa kwa dunia iwe paradiso. Je, naweza kukusomea kile ambacho nabii huyo aliandika? [Soma Isaya 11:6-9.] Unabii huu hunifanya nifikirie kuhusu nukuu moja katika Kurani ambalo lapatikana katika broshua hii.” Fungua ukurasa wa 9 katika broshua Guidance of God, na usome nukuu lililochapwa kwa herufi nzito, ambalo hutaja waadilifu wakiimiliki dunia. Akionyesha kupendezwa, endelea kuzungumzia fungu la 7 hadi 9 kwenye ukurasa ule mwingine. Mwachie broshua, na upange kufanya ziara ya kurudia.—Ili kupata utoaji mwingine, ona Huduma ya Ufalme Yetu ya Februari 1998, ukurasa wa 6, fungu la 27.
9 Unapomwalika mtu mchunguze broshua Guidance of God, ni afadhali kutumia neno mazungumzo, si funzo la Biblia. Mnapomaliza broshua hiyo, mwanafunzi apaswa kuwa tayari kujifunza broshua Anataka au kitabu Ujuzi. Vichapo vingine ambavyo vimekusudiwa Waislamu hasa ni trakti Jinsi ya Kuipata Barabara ya Kwenda Kwenye Paradiso na kijitabu Sasa Ndio Wakati wa Kumtii Mungu Kweli Kweli.
10 Kukiwa na ujuzi huu kuhusu itikadi za Kiislamu na hisi zao, twaweza kutumia utambuzi tunapochagua fasihi tutakazowatolea Waislamu na kwa njia hiyo twawatolea ushahidi. Yehova na aendelee kubariki jitihada zetu za kusaidia watu wa aina zote waliitie jina lake ili waokolewe.—Mdo. 2:21.