“Wajaribiwe Juu ya Kufaa”—Jinsi Gani?
1 Kwa kuwa ukuzi unaendelea katika tengenezo la Yehova, kuna uhitaji wa daima wa akina ndugu wanaostahili kutumikia wakiwa watumishi wa huduma. Ndugu wengi ambao hawajawekwa rasmi, kutia ndani matineja, wana tamaa ya kutumika katika kutaniko. Wanapogawiwa kazi za ziada, wao huhisi kwamba wanahitajika na wanaona kuwa wametimiza jambo fulani. Ili wafanye maendeleo zaidi itategemea ikiwa ‘watajaribiwa juu ya kufaa.’ (1 Tim. 3:10) Hilo hutimizwaje?
2 Daraka la Wazee: Kwa kuongezea kumpima ndugu kwa kutumia sifa za Kimaandiko zilizo katika 1 Timotheo 3:8-13, wazee watamjaribu ndugu huyo kuona ikiwa anafaa kutwaa madaraka. Huenda wakampa mgawo wa kugawanya magazeti na vichapo, kushughulikia vikuza-sauti, kudumisha Jumba la Ufalme, na kadhalika. Wazee wataangalia jinsi anavyoitikia na kutunza migawo yake. Watatafuta sifa kama vile kutegemeka, kufika kwa wakati, bidii, kiasi, utayari, na kupatana na wengine. (Flp. 2:20) Je, anaweka kielelezo katika mavazi na mapambo yake? Je, yeye huchukua madaraka kwa uzito? Wanataka kuona katika “mwenendo wake bora kazi zake kwa upole ulio wa hekima.” (Yak. 3:13) Je, kweli anajitahidi kufikia mapendeleo ili kusaidia kutaniko? Je, anatekeleza amri ya Yesu ya ‘kufanya wanafunzi’ kwa kushiriki kwa bidii katika huduma ya shambani?—Mt. 28:19; ona Mnara wa Mlinzi, Septemba 1, 1990, ukurasa wa 18-28.
3 Ingawa hakuna kiwango cha chini zaidi cha umri kilichowekwa ili kumweka mtu rasmi kuwa mtumishi wa huduma, Biblia huwataja ndugu hao kuwa “watu wahudumuo.” Hatungetarajia wawe katika umri wa mapema wa ujanani, hasa kwa sababu uwezekano wa kuwa na mke na watoto umetajwa. (1 Tim. 3:12, 13) Wanaume hao hawapaswi kushindwa na “tamaa zenye kutukia ujanani” bali wapaswa kujiendesha wenyewe kwa uangalifu, wakiwa na msimamo mzuri na dhamiri safi mbele za Mungu na wanadamu.—2 Tim. 2:22.
4 Ingawa uwezo wa asili unafaa, jambo la maana zaidi ni mtazamo na nia ya mtu. Je, ndugu huyo anatamani kwa unyenyekevu kumsifu Mungu na kuwatumikia ndugu zake? Ikiwa ndivyo, Yehova atabariki jitihada zake za kufanya maendeleo kutanikoni.