Je, Wahubiri kwa Ujasiri?
1 Licha ya kukamatwa na kutishwa na wapinzani, Petro na Yohana waliendelea kutangaza ujumbe wa Ufalme kwa ujasiri. (Mdo. 4:17, 21, 31) Kuhubiri kwa ujasiri humaanisha nini kwetu leo?
2 Kutoa Ushahidi kwa Ujasiri: Neno sawa na “jasiri” ni “hodari,” ambalo humaanisha “kutokuwa na hofu kabisa, kuwa thabiti, na kuvumilia.” Kwa Wakristo wa kweli, kuhubiri kwa ujasiri humaanisha kutoogopa kuongea kwa uhuru wakati wowote kunapokuwa na fursa inayofaa ya kuwaambia wengine habari njema. (Mdo. 4:20; 1 Pet. 3:15) Humaanisha kwamba hatuaibikii habari njema. (Zab. 119:46; Rom. 1:16; 2 Tim. 1:8) Hivyo, ujasiri ni sifa inayohitajiwa ili kutimiza utume wetu wa kuhubiri habari njema za Ufalme wakati huu wa mwisho. Hutusukuma kuwaambia watu habari njema popote wanapoweza kupatikana.—Mdo. 4:29; 1 Kor. 9:23.
3 Ujasiri Shuleni: Je, mwelekeo wa kuhofu au kuona haya hufanya iwe vigumu kwako kuhubiria wanashule wenzako? Nyakati nyingine si rahisi; kwa kweli hilo laweza kuwa jambo gumu sana. Hata hivyo, Yehova atakuimarisha ukimwomba akupe ujasiri wa kuhubiria wengine. (Zab. 138:3) Ujasiri utakusaidia kujitambulisha mwenyewe kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova na kustahimili dhihaka. Tokeo litakuwa kwamba, kuhubiri kwako shuleni labda kutaokoa wale watakaokusikiliza.—1 Tim. 4:16.
4 Ujasiri Kazini: Je, wajulikana kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova kazini? Njia pekee ambayo wafanyakazi wenzako wanaweza kufikiwa na habari njema huenda ikawa ni unapowahubiria. Ujasiri wako pia utakusaidia uombe ruhusa ya kuhudhuria mikutano yako ya Kikristo na mikusanyiko.
5 Ujasiri Unapokuwa Majaribuni: Kujipa ujasiri ni muhimu tunapokabili upinzani. (1 The. 2:1, 2) Hutusaidia kushikilia imani yetu tunapotishwa, tunapodhihakiwa, au kunyanyaswa. (Flp. 1:27, 28) Hutuimarisha kusimama imara chini ya msongo wa kuridhia uaminifu wetu kwa viwango vya Mungu wetu, Yehova. Hutuimarisha kudumisha amani yetu wengine wanapozusha mabishano.—Rom. 12:18.
6 Hata tukabili magumu ya aina gani, na tuvumilie katika kuhubiri habari njema kwa ujasiri.—Efe. 6:18-20.