Mikusanyiko Ni Wakati wa Shangwe!
1 Mikusanyiko ya Mashahidi wa Yehova ni nyakati za shangwe. Kwa zaidi ya miaka 100, mikusanyiko hii imechangia ongezeko ambalo limekuwa likiendelea katika tengenezo letu. Tumeona baraka tele za Yehova kwenye kazi yetu ya ulimwenguni pote, tangu hatua za kwanza-kwanza. Kwenye mkusanyiko wetu wa kwanza wa siku za kisasa, huko Chicago, Illinois, mwaka wa 1893, jumla ya watu 70 kati ya 360 waliohudhuria walibatizwa kwa kuonyesha wakfu wao kwa Yehova. Mikusanyiko ya mwaka uliopita ya “Watekelezaji wa Neno la Mungu” ilikuwa na jumla ya hudhurio la ulimwenguni pote la watu 9,454,055, na 129,367 wakabatizwa. Hiyo yatuletea shangwe iliyoje!
2 Tangu nyakati za Biblia, mikusanyiko ya watu wa Mungu imeandaa njia inayojulikana sana ya kufunza mafundisho ya Yehova. Nyakati za Ezra na Nehemia, watu walisikiliza Sheria ikisomwa “tangu mapambazuko hadi adhuhuri.” (Neh. 8:2, 3) Kwa sababu ya kupata uelewevu mzuri juu ya Sheria wakati huo, watu wakawa na “furaha nyingi.” (Neh. 8:8, 12) Sisi pia twashangilia kwa kuwa mikusanyiko hutupa fursa ya kupokea mafundisho na chakula cha kiroho “kwa wakati unaofaa” kutoka kwa Yehova kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45) Kwa kuwa Yesu alisema kwamba mwanadamu lazima aishi “kwa kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova,” mikusanyiko ni muhimu kwa hali yetu ya kiroho.—Mt. 4:4.
3 Yafaa Tujitahidi Kuhudhuria: Sisi sote twapaswa kufanya uwe mradi wetu kuhudhuria siku zote za Mkusanyiko wa Wilaya wa mwaka huu wa “Walimu wa Neno la Mungu.” Twapaswa kupanga kufika mapema kila siku na kubaki hadi tujiunge katika kusema “Amina!” baada ya sala ya kumalizia. Ili tutimize hayo huenda tukahitaji kurekebisha ratiba yetu. Kuomba ruhusa kazini ili kuhudhuria mkusanyiko kwaweza kuwa jambo gumu. Twahitaji kuchukua msimamo imara, bila kutazamia kwamba inawezekana tu kupata ruhusa. Ikiwa twahitaji mahali pa kulala na/au usafiri, twapaswa kufanya mipango mapema. Jitihada zozote tutakazofanya zitafaa!
4 Watu wa Yehova hawalinganishi baraka za kuhudhuria mkusanyiko na pesa. Angalia vielelezo vya wengine ambao waliazimia kuhudhuria Kusanyiko la Wilaya la Mashahidi wa Yehova la Mapenzi ya Kimungu huko New York City mwaka wa 1958. Ndugu mmoja alifunga biashara yake ya ujenzi kwa majuma mawili ili ajitolee kusaidia na kuhudhuria kusanyiko. Ndugu mmoja kutoka Visiwa vya Virgin aliuza shamba lake la ekari tano ili familia yake yote ya watu sita wahudhurie kusanyiko hilo. Wenzi wa ndoa wachanga waliuza mashua yao ili wao na watoto wao watatu wenye umri wa kuanzia miezi miwili hadi miaka saba waende kwenye kusanyiko hilo. Ndugu watatu wa kimwili kutoka California waliambiwa kwamba ikiwa watakosekana kazini mwao, hawatazipata watakaporudi. Hata hivyo, hilo halikuwafanya wasiende kwenye kusanyiko hilo lisilosahaulika. Huku kwetu, akina ndugu na dada wameuza ng’ombe, mbuzi, na kondoo au mazao ili wahudhurie mikusanyiko.
5 Yehova Huthawabisha Jitihada Zetu: Yehova huona na kubariki jitihada za watu wake. (Ebr. 6:10) Kwa mfano, katika Kusanyiko la Ongezeko la Kitheokrasi la 1950, wale waliohudhuria walisikiliza hotuba yenye kutokeza “Mifumo Mipya ya Mambo.” Ndugu Frederick Franz aliamsha na kuchochea upendezi wa wote kwa kuuliza hivi: “Je, kusanyiko hili la kimataifa litafurahi kujua kwamba hapa leo hii, miongoni mwetu, kuna idadi ya wale wanaotazamiwa kuwa wakuu wa dunia mpya?” Sasa miaka 50 ikiwa imepita, tungali twashangilia uelewevu huo ulio wazi wa Zaburi 45:16.
6 Baada ya kuhudhuria mkusanyiko wa wilaya wa mwaka jana, ndugu mmoja aliye kichwa cha familia aliandika hivi kwa uthamini: “Akina ndugu, hamwezi kuwazia jinsi mkusanyiko huu ulivyokuwa wenye kuokoa uhai. Familia yangu ilihamia jijini kwa sababu ya kazi ya kuajiriwa, ingawa hivyo, hali yetu ya kiroho ikadhoofika. . . . Tulikuwa tumepuuza wajibu wetu wa Kikristo. Hata tuliacha kuhudhuria mikutano na kushiriki katika utumishi. . . . Kusanyiko hili limetutia nguvu tena, na tunaweka miradi ya kiroho na kujitayarisha kuitimiza.”
7 Yehova anatuandalia chakula cha kiroho tunachohitaji. Yeye huandaa meza yenye vinono kwenye mikusanyiko yetu. Uthamini wetu kwa uandalizi huu wapaswa kutuwezesha kusema kama alivyosema Kornelio alipotembelewa na mtume Petro: “Wakati huu sisi tupo sote mbele ya Mungu kuyasikia mambo yote ambayo umeamriwa na Yehova kusema.” (Mdo. 10:33) Na tuufanye uwe mradi wetu ‘kuwapo mbele ya Mungu’ katika kila kipindi cha Mkusanyiko wa Wilaya wa mwaka huu “Walimu wa Neno la Mungu” na tushangilie!