Jitayarishe Kujifunza Unabii wa Isaya!
1 “Waabudu waaminifu waweza kuwa na uhakika kwamba Yehova . . . hatauruhusu ulimwengu wa Shetani uendelee kuwapo hata kwa siku moja zaidi kupita ilivyo haki.” Hayo ni maelezo yenye kutia moyo kama nini! Yamenukuliwa kutoka wapi? Kitabu Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote I. Je, unabii wa Isaya watupa sababu ya kufikia mkataa huo wenye kutia moyo? Ndiyo! Katika kitabu hicho cha Biblia, habari kuu ya wokovu imekaziwa waziwazi. (Isa. 25:9) Ndiyo sababu litakuwa jambo lenye kutia moyo sana kujifunza sehemu hii ya Neno la Mungu kwenye Funzo la Kitabu la Kutaniko. Je, tutahudhuria ili kulifurahia kila juma? Kwa nini tuhudhurie?
2 Kwenye Isaya 30:20, NW, Yehova anaitwa “Mfunzi Mtukufu.” Kila Mkristo apaswa kusikiliza kwa makini Yehova atufunzapo kupitia Neno lake na kupitia vichapo vya Biblia vilivyotolewa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45; Isa. 48:17, 18) Kitabu cha Unabii wa Isaya I ni mojawapo ya vichapo hivyo. Waweza kunufaikaje zaidi kutokana na kujifunza kitabu hicho?
3 Jitayarishe Ili Ushiriki: Kila juma tenga wakati wa kutosha ili kutayarisha funzo la kitabu. Soma kila fungu. Fikiria kila swali. Tia alama majibu katika kitabu chako. Maandiko yaliyonukuliwa kutoka Isaya yamechapwa kwa herufi nzito. Yasome kwa uangalifu. Kwa habari ya maandiko yale mengine yaliyowekwa bila kunukuliwa, yasome uone jinsi yanavyohusiana na habari hiyo. Tafakari yale unayojifunza. Kisha shiriki maelezo uliyotayarisha pamoja na kikundi chenu cha funzo la kitabu.
4 Ndugu anayeongoza funzo la kitabu apaswa kusaidia wote wanaohudhuria watumie Biblia zaidi na kuona jinsi wanavyoweza kutumia habari inayochunguzwa. Ukipewa fursa ya kwanza kujibu, toa maelezo rahisi na ya moja kwa moja. Ikiwa tayari mtu amejibu hivyo, waweza kuongezea maana inayozungumziwa. Labda waweza kuonyesha jinsi andiko la msingi linavyounga mkono habari kuu. Jaribu kutoa maelezo kwa maneno yako mwenyewe, na ufurahie kushiriki katika mazungumzo.
5 Acheni tuchunguze pamoja kwa hamu ujumbe wenye thamani wa kitabu cha Isaya. Utatutia moyo tuishi kila siku tukitazamia kwa shangwe wokovu wa Yehova!—Isa. 30:18.