Je, Unatumia Yale Uliyojifunza Katika Mkusanyiko wa Wilaya wa “Walimu wa Neno la Mungu”?
1 Yeyote aliyehudhuria mkusanyiko wa wilaya wa mwaka huu aliona kwamba watu wa Yehova walinuia kutimiza utume wao wa kufundisha Neno la Mungu. (Mt. 28:19, 20) Uliporudi nyumbani, ni mambo gani hasa uliyojifunza ambayo uliazimia kutumia katika maisha yako na katika huduma ya shambani?
2 Maandiko Yaliyopuliziwa Ni Yenye Manufaa kwa Kufundisha: Kichwa cha siku ya kwanza kilikazia 2 Timotheo 3:16. Hotuba ya msingi ilionyesha kwamba tukiwa “Tumeandaliwa Kikamili Kuwa Walimu wa Neno la Mungu,” lazima tuheshimu sana Neno la Mungu kuliko maoni yoyote ya binadamu au desturi, na kulitumia daima. Lazima pia tusali kila siku tupate roho takatifu ili itusaidie katika huduma yetu na kujitahidi kusitawisha tunda lake kuu—upendo. Na tukiwa wahudumu ni lazima turuhusu tengenezo la Yehova la kidunia litufundishe kupitia mikutano yote ya kutaniko.
3 Ule mfululizo wa hotuba uliotolewa Ijumaa wenye kichwa, “Tujifunze Tunapowafundisha Wengine,” ulieleza kwamba lazima tuwe mfano bora katika (1) kuzingatia sheria za Mungu katika sehemu zote za maadili ya Kikristo, (2) kudumisha mazoea mazuri ya kujifunza, na (3) kuondoa mitazamo na hali za moyo na akili ambazo Ibilisi anaweza kutumia. Halafu, tulijifunza jinsi ya kulinda familia zetu kutokana na dhara la ulimwengu la ponografia. Wazazi walisihiwa kuweka kielelezo bora kwa kuepuka kutazama hata kidogo vipindi vyovyote vinavyoonyesha picha chafu na wachunguze watoto wao wanapotumia Internet na wanapotazama televisheni. Ni madokezo gani ya programu ya siku ya Ijumaa ambayo umeanza kutumia?
4 Hotuba ya mwisho siku hiyo ilizidisha azimio letu la kuthamini nuru ya Yehova, na kushikamana na jamii ya watiwa-mafuta wa Mungu wenye uaminifu, na kuendeleza amani ya watu wa Yehova. Je, umesoma kitabu kipya cha Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote II?
5 Wenye Sifa za Ustahili wa Kutosha Kufundisha Wengine: Kichwa cha siku ya pili kilitegemea 2 Timotheo 2:2. Uliposikiliza mfululizo wa Jumamosi asubuhi, je, uliandika madokezo ya jinsi ya (1) kutafuta kabisa wale wanaostahili, (2) kuendeleza upendezi wao, na (3) kuwafundisha kushika mambo yote ambayo Kristo aliamuru? Je, unatumia yale uliyojifunza—kuonyesha wenye nyumba angalau jambo moja katika Maandiko ili kuweka msingi wa ziara ya kurudia?
6 Kisha programu ya alasiri ikakazia umuhimu wa kumwiga Mwalimu Mkuu, Yesu. Ni katika njia zipi wewe hujitahidi kufanya kama alivyofanya? Kutokana na yale uliyojifunza katika mfululizo wa siku hiyo, unawezaje ‘Kufaidika Zaidi na Elimu ya Kitheokrasi’? Ni madokezo gani ambayo umetumia kuongeza uwezo wako wa kukaza fikira wakati wa funzo la kibinafsi na mikutano ya kutaniko?
7 Bila shaka, kichapo kipya kitakachokuja chenye kichwa, Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi kitatusaidia tukuze uwezo wetu tukiwa wasemaji na walimu wa Neno la Mungu. Uangalifu mkubwa utakaziwa katika sifa za usemi ambazo watumishi wa Mungu wa nyakati za Biblia walikuwa nazo. Kila somo katika kitabu hicho kipya lina masanduku ambayo yanaonyesha wazi kile tunachohitaji kufanya, kwa nini ni cha maana, na jinsi ya kukifanya. Mazoezi yenye faida yanatiwa ndani. Akina dada watakuwa na vikao 29 ambavyo wanaweza kuchagua mojawapo ya vikao hivyo wanapotoa hotuba zao. Baada ya muda, mabadiliko yaliyotangazwa kuhusu mpangilio wa shule yatafanywa. Je, una ratiba nzuri ya kawaida ya kujifunza na kutayarisha ili ufaidike kikamili kutokana na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi kila juma?
8 Iweni Walimu kwa Kufikiria Wakati: Andiko la Waebrania 5:12 lilitayarisha akili za wasikilizaji Jumapili. Mfululizo wa asubuhi, “Unabii wa Malaki Hututayarisha kwa Ajili ya Siku ya Yehova,” ulitusihi tumpe Mungu yaliyo bora kabisa na kuchukia aina zote za hiana ili tuokoke siku kuu ya Yehova yenye kuogofya. Drama yenye kichwa, “Heshimu Mamlaka ya Yehova,” ilionyesha kwa mkazo jinsi kiburi, tamaa ya makuu, wivu, na uaminifu usiofaa wa Kora na washiriki wake ulivyoongoza kwenye uasi wa waziwazi dhidi ya Yehova mwenyewe. Hotuba iliyofuata ilikazia uhitaji wa kunyenyekea mamlaka ya kimungu katika familia na kutaniko katika siku zetu. Hotuba ya watu wote yenye kichwa, “Ni Nani Wanaofundisha Mataifa Yote Ile Kweli?” ilithibitisha kwamba Mashahidi wa Yehova ndio wanaofanya hivyo tofauti na Jumuiya ya Wakristo, ambayo hudai eti inafundisha kweli ya Biblia.
9 Ni wazi kwamba Yehova anatufundisha jinsi ya kuwa walimu bora wa Neno lake. Na tutumie yale tuliyojifunza, ‘tukikaza uangalifu kwetu wenyewe na kwa kufundisha kwetu, ili tujiokoe wenyewe na wale wanaotusikiliza pia.’—1 Tim. 4:16.