“Nitapata Wapi Wakati?”
1 Wengi wetu hulalamika hivyo kwani tuna shughuli nyingi sana. Imesemwa kwamba wakati ndicho kitu cha maana zaidi maishani na kinachopita upesi zaidi. Kwa hiyo twaweza kupata wapi wakati ili kufanya mambo ya maana zaidi, kama vile kusoma na kujifunza Neno la Mungu?—Flp. 1:10.
2 Suluhisho si kupata wakati zaidi, bali ni kuamua tunachotaka kufanya na wakati tulio nao. Sote tuna saa 168 kila juma, na huenda tukatumia saa 100 kulala na kufanya kazi. Kwa hiyo twawezaje kutumia saa zinazobaki kwa manufaa? Andiko la Waefeso 5:15-17 hupendekeza tutembee ‘si kama wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, tukijinunulia kabisa wakati unaofaa, tukifahamu mapenzi ya Yehova ni nini.’ Hiyo yaonyesha kwamba twapaswa kutumia kikamili kila fursa kufanya mambo ambayo Yehova anasema ni muhimu.
3 Yesu alilinganisha siku zetu na zile za Noa. (Luka 17:26, 27) Katika siku hizo, watu walikuwa na shughuli nyingi za maisha. Hata hivyo, Noa alipata wakati wa kujenga safina kubwa sana na kuhubiri. (Ebr. 11:7; 2 Pet. 2:5) Jinsi gani? Kwa kutanguliza mapenzi ya Mungu na kumtii kwa kufanya mambo ‘sawasawa na alivyoamriwa.’—Mwa. 6:22.
4 Ni Nini Kinachopasa Kutangulizwa? Yesu alisema: “Binadamu lazima aishi, si kwa mkate pekee, bali kwa kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova.” (Mt. 4:4) Kila juma, sisi hupokea ‘kipimo cha magawio ya chakula kwenye wakati ufaao.’ (Luka 12:42) Hilo lataka tuwe na ratiba ya kusoma na kujifunza kwa ukawaida ili tuelewe habari zote hizo na kufaidika. Tukithamini chakula cha kiroho, hatutakisoma haraka-haraka kama vile mtu anavyoweza kula chakula cha kimwili mbiombio. Badala yake, uthamini wetu utatuchochea tutumie wakati kujifunza na kufurahia mambo ya kiroho.
5 Twaweza kupata uhai udumuo milele tukiendelea kula chakula cha kiroho. (Yn. 17:3) Tunahitaji kutanguliza jambo hilo katika ratiba yetu ya kila siku. Je, twaweza kupata wakati wa kusoma Biblia kila siku na kutayarisha mikutano ya Kikristo? Naam, twaweza. Kisha tutapokea “thawabu nyingi” zinazotokana na kujua na kufanya mapenzi ya Mungu.—Zab. 19:7-11.