Baraka Tunazopata kwa Kuthamini Upendo wa Yehova—Sehemu ya 1
1 Mtume Yohana aliandika hivi: “Kwa habari yetu, twapenda, kwa sababu [Yehova] alitupenda sisi kwanza.” (1 Yoh. 4:19) Tunapofikiria mambo yote ambayo Yehova ametupatia, tunachochewa kumthamini sana. Yesu aliweka mfano kwa kutii na kutoa ushahidi kuhusu jina la Mungu na Ufalme wake. (Yn. 14:31) Inafaa kuchunguza baadhi ya njia za kuthamini upendo wa Yehova na baraka tunazopata kwa kufanya hivyo.
2 Kwenda Nyumba Hadi Nyumba: Yesu aliwafundisha wanafunzi wake jinsi ya kuhubiri kuhusu Ufalme. Maagizo yake yaonyesha wazi kwamba wanafunzi walienda nyumba hadi nyumba, wakitangaza habari njema. (Luka 9:1-6; 10:1-7) Kumpenda Mungu na jirani hutuwezesha kuendelea kuhubiri ijapokuwa ubaridi na upinzani. Hata hivyo, sisi wenyewe hunufaika kwani imani na usadikisho wetu huimarika, na tumaini letu kuzidishwa.
3 Tumewapata watu wengi wenye njaa na kiu ya kweli huku tunapofanya kazi chini ya mwelekezo wa malaika. (Ufu. 14:6) Wenye-nyumba wamesema kwamba kabla ya Shahidi kuwatembelea walikuwa wakisali ili wapate msaada. Mashahidi wawili pamoja na mtoto mchanga walikuwa wakihubiri nyumba hadi nyumba kwenye kisiwa kimoja cha Karibea. Dada hao walipoamua kumaliza mahubiri, mtoto huyo alienda peke yake kwenye mlango uliofuata na kubisha. Msichana mmoja akafungua mlango. Dada hao walipoona hilo, walienda kuzungumza naye. Aliwakaribisha na akawaeleza kwamba alikuwa ametoka tu kusali ili Mungu awatume Mashahidi wamfundishe Biblia!
4 Kutoa Ushahidi Barabarani: Kwa kuwa ni vigumu kuwapata watu nyumbani katika maeneo fulani, kutoa ushahidi barabarani ni njia bora ya kuwahubiria watu. Isitoshe, watu wengi huishi katika majengo yenye malango au yenye ulinzi mkali, mahali ambapo hatuwezi kuhubiri nyumba hadi nyumba. Hata hivyo, uthamini wetu kwa upendo wa Yehova hutuchochea kutumia kikamili njia zozote zile ili kuwapa watu ujumbe wa Ufalme, kutia ndani kutoa ushahidi barabarani.—Mit. 1:20, 21.
5 Kufanya Ziara za Kurudia: Kwa kuwa tunawatafuta wale ‘wanaoona uhitaji wao wa kiroho,’ tunataka kufanya yote tuwezayo ili kutosheleza uhitaji huo. (Mt. 5:3) Hilo latia ndani kurudi ili kutia maji mbegu za kweli tulizopanda. (1 Kor. 3:6-8) Dada mmoja nchini Australia alimwachia trakti mwanamke mmoja aliyeonekana hapendezwi. Hata hivyo, dada huyo aliendelea kujaribu kumpata tena. Alipompata mwishowe, dada yetu aligundua kwamba baada ya ziara ya kwanza, mwanamke huyo alinunua Biblia ya bei ghali. Dada huyo akaanza kujifunza naye!
6 Kuongoza Mafunzo ya Biblia: Hii yaweza kuwa sehemu yenye kufurahisha na kuridhisha zaidi ya huduma yetu. Ni baraka kama nini kuwasaidia watu kujifunza kumhusu Yehova, kuona wakifanya mabadiliko maishani mwao ili kumpendeza, kisha kushuhudia ubatizo wao wa Kikristo wanapoonyesha wakfu wao kwa Mungu!—1 The. 2:20; 3 Yoh. 4.
7 Katika toleo linalofuata, tutachunguza baraka nyingine tunazopata kwa kuthamini upendo wa Yehova.