Baraka Tunazopata kwa Kuthamini Upendo wa Yehova—Sehemu ya 2
1 Mwezi uliopita, tulikazia njia nne tunazoweza kuonyesha tunathamini upendo wa Yehova katika huduma. (1 Yoh. 4:9-11) Tutaongeza njia nyingine tano tunazoweza kufanya hivyo. Sisi hupata baraka tunaposhiriki kikamili kusaidia wengine kiroho.
2 Kutoa Ushahidi wa Vivi Hivi: Hii ni njia yenye matokeo ya kupata watu walio na njaa na kiu ya uadilifu na kuwaachia vichapo vinavyoweza kuwasaidia. Inafaa ‘kununua wakati unaofaa’ ili nyakati zote tuhubirie yeyote tunayekutana naye. (Efe. 5:16) Tunapotembelea watu wa ukoo tunaweza kutafuta njia fulani za kuwahubiria. Huenda tukahitaji kuwa hodari ili tuweze kuwahubiria, lakini ikiwa tunathamini upendo wa Yehova na kuelewa uhitaji wa watu, tutahubiri kila tupatapo fursa ya kufanya hivyo.—2 Tim. 1:7, 8.
3 Mishonari mmoja alibarikiwa kwelikweli kwa sababu alianzisha mazungumzo na msafiri mwenzake kwenye taksi moja. Mwanamume huyo alipendezwa. Ziara za kurudia zikafanywa na funzo la Biblia likaanzishwa. Mwanamume huyo alikubali kweli na kufanya maendeleo kufikia kuwa mzee wa kutaniko!
4 Kuandika Barua: Labda hatuwezi kwenda nyumba hadi nyumba kwa sababu ya ugonjwa au hali mbaya ya hewa. Twaweza kuandika barua, tukitoa ushahidi mfupi kwa watu tunaowajua, wale ambao wamepoteza wapendwa wao katika kifo, au wale ambao hawakuwa nyumbani tulipokuwa katika eneo. Twaweza kutia ndani mojawapo ya trakti zetu ambayo ina ujumbe wa Biblia wenye kuvutia na inayomtia moyo mwenye kuipokea aandike ikiwa ana maswali yoyote. Tumia anwani yako ya kibinafsi au ya Jumba la Ufalme; tafadhali usitumie anwani ya ofisi ya tawi.
5 Kutoa Ushahidi Kupitia Simu: Hii ni njia nzuri ya kufikia watu katika miji na majiji makubwa ambao hatuwapati tunapohubiri nyumba hadi nyumba. Tukifanya hivyo kwa busara, kwa fadhili, na ustadi, huenda tukapata matokeo mazuri.
6 Wakati dada mmoja alipokuwa akihubiri kwa simu, alimwuliza mwanamke mmoja kama amewahi kufikiria kuhusu wakati wake ujao na wa familia yake. Mwanamke huyo alikubali kuwa amefikiria jambo hilo. Alieleza kwamba, kwa sababu ya kukata tamaa alijitenga na kukaa nyumbani. Akichochewa na hangaikio la kweli la dada huyo, mwanamke huyo alikubali kukutana naye kwenye soko lililokuwa karibu. Matokeo yakawa kwamba, mwanamke huyo alikubali funzo la Biblia!
7 Kuwakaribisha Wageni: Ikiwa twapenda jirani zetu, tutakuwa macho kumkaribisha mgeni anayekuja kwenye mikutano yetu. (Rom. 15:7) Mfanye aone kuwa yumo miongoni mwa watu wanaojali sana hali yake ya kiroho. Tukimjali sana na kumwalika awe na funzo la Biblia huenda akachochewa kukubali msaada wetu.
8 Mwenendo Wetu Mzuri: Kupitia mwenendo wetu mzuri, twapamba ile kweli. (Tito 2:10) Watu wa ulimwengu wanapotusifu tukiwa Mashahidi wa Yehova, wanamletea Mungu wetu heshima. (1 Pet. 2:12) Hiyo pia itasaidia wengine waifuate ile njia ya uhai.
9 Kwa nini usichunguze njia hizo tano za kuonyesha uthamini wetu kwa upendo mwingi ambao Yehova ametuonyesha na tutende kulingana nazo? (1 Yoh. 4:16) Ukifanya hivyo, utapokea baraka nyingi mno.