Wakumbuke Waaminifu Wenye Umri Mkubwa Zaidi
1 Ajapokuwa mjane na mzee, Ana mwenye umri wa miaka 84 “alikuwa hakosi kamwe kuwa katika hekalu.” Yehova alimbariki kwa njia ya pekee kwa sababu ya uaminifu wake. (Luka 2:36-38) Leo, ndugu na dada wengi huonyesha roho kama ya Ana wajapokabili magumu. Nyakati nyingine huenda waaminifu hao wakavunjika moyo wanapokabiliana na matatizo ya afya au udhaifu fulani unaosababishwa na uzee. Na tuchunguze baadhi ya njia zifaazo ambazo twaweza kuwatia moyo na kuwasaidia wadumishe ratiba nzuri ya kiroho.
2 Mikutano na Huduma: Waaminifu wengi wenye umri mkubwa zaidi wanaweza kwa urahisi kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida wengine wakijitolea kwa upendo kuwabeba kwa gari. Kufanya hivyo huwajenga kiroho waaminifu hao ambao wametumikia kwa muda mrefu na hunufaisha pia kutaniko. Je, umeshiriki kazi hiyo njema?—Ebr. 13:16.
3 Wakristo wa kweli hupata shangwe na uradhi wanaposhiriki kwa ukawaida katika huduma. Lakini kufanya hivyo si rahisi kwa walio na umri mkubwa zaidi na walio dhaifu. Je, inawezekana wapendwa hawa waandamane nawe wakiwa ‘wafanyakazi wenzako’ katika kazi ya kuhubiri? (Rom. 16:3, 9, 21) Labda unaweza kumkaribisha aende nawe kwenye ziara ya kurudia au funzo la Biblia. Ikiwa mwenye umri mkubwa zaidi hawezi kutoka nyumbani, unaweza kupanga ili mwanafunzi wa Biblia aje nyumbani kwa ndugu au dada huyo ili mjifunzie huko?
4 Funzo na Ushirika: Mara kwa mara, wengine humwalika mtu mwenye umri mkubwa zaidi au aliye dhaifu kimwili ahudhurie funzo lao la familia, hata hufanyia funzo hilo nyumbani mwa watu hao. Mama mmoja alipeleka watoto wake kwenye nyumba ya dada mmoja mwenye umri mkubwa zaidi ili wafanye funzo lao la Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, na wote walitiwa moyo sana na ushirika huo. Watu hao huthamini pia wakialikwa kwenye mlo au tafrija. Ikiwa walio dhaifu kimwili hawawezi kutembelea watu, labda unaweza kuwatembelea kwa ufupi na kujitolea kuwasomea, kusali pamoja nao, au kuwaeleza mambo yaliyoonwa yenye kujenga.—Rom. 1:11, 12.
5 Yehova huwathamini waaminifu hao wenye umri mkubwa zaidi. (Ebr. 6:10, 11) Twaweza kumwiga kwa kuwaheshimu na kuwasaidia wadumishe ratiba nzuri ya kiroho.