Sanduku La Swali
◼ Kikundi kinachosema lugha ya kigeni kinapaswa kuanzishwa wakati gani?
Eneo la kutaniko linapokuwa na watu wengi wenye kuongea lugha ya kigeni, wazee wanapaswa kufanya yale wanayoweza ili kupanga kazi ya kuhubiri katika lugha hiyo. (km 2/98 uku. 3-4) Huenda ikawa kwamba watu wanaosema lugha ya kigeni wametapakaa kote katika maeneo ya makutaniko mawili au zaidi katika ujirani. Ikiwa hivyo, mwangalizi au waangalizi wa mzunguko watatoa mwelekezo unaohitajiwa, wakisaidia makutaniko yanayohusika yashirikiane katika kazi ya kuhubiri. Mara kwa mara, hotuba ya watu wote au Funzo la Mnara wa Mlinzi laweza kupangwa ili kuona ni watu wangapi wanaohudhuria mikutano ya lugha hiyo ya kigeni.
Kikundi cha lugha ya kigeni chaweza kuanzishwa wakati matakwa yafuatayo yanapotimizwa: (1) Kuna wahubiri au watu wenye kupendezwa ambao wanaelewa habari njema katika lugha ya kigeni. (2) Kuna mzee au mtumishi wa huduma anayestahili ambaye anaweza kuongoza angalau mkutano mmoja kila juma. (3) Baraza la wazee liko tayari kutegemeza kikundi hicho. Matakwa hayo yanapotimizwa, wazee wanapaswa kujulisha ofisi ya tawi ili kikundi hicho kitambuliwe rasmi na maagizo zaidi yatolewe.
Vikundi vingi huanza kwa kufanya Funzo la Kitabu la Kutaniko kila juma. Baadaye, wazee wanaweza kukubali kuongeza mikutano mingine, kama vile Hotuba ya Watu Wote na Funzo la Mnara wa Mlinzi. Hotuba Namba 2, 3, na 4 za Shule ya Huduma ya Kitheokrasi zaweza kutolewa katika darasa tofauti ikiwa kuna mzee au mtumishi wa huduma anayeifahamu lugha hiyo vizuri na ambaye anaweza kutoa mashauri. Lakini, kikundi hicho kitajiunga na kutaniko kusikiliza hotuba ya sifa ya usemi, hotuba ya maagizo, mambo makuu ya usomaji wa Biblia, na Mkutano wa Utumishi. Pia kikundi hicho kinaweza kuwa na mikutano yao ya utumishi wa shambani.
Wote katika kikundi hicho watashirikiana sana na baraza la wazee. Wazee wanapaswa kutoa mwelekezo na kuchukua hatua ya kutunza mahitaji ya kikundi hicho. Mwangalizi wa mzunguko anapotembelea kutaniko linalotegemeza kikundi hicho, atapanga pia kuhubiri pamoja na kikundi hicho ili kukijenga kiroho. Kwa baraka za Yehova, huenda kikundi hicho cha lugha ya kigeni kikawa kutaniko baada ya muda fulani.