Unatanguliza Nini Maishani Mwako?
1 Mashirika mengi ya kidini yanatilia maanani kuwasaidia watu hasa kwa kujenga na kugharimia ujenzi wa shule au hospitali. Hata hivyo, ingawa Mashahidi wa Yehova hawasahau “kutenda mema na kule kushiriki vitu pamoja na wengine,” jambo kuu maishani mwao ni kuwasaidia watu kiroho.—Ebr. 13:16.
2 Mfano wa Wakristo wa Karne ya Kwanza: Yesu alifanya mambo mengi mema katika huduma yake duniani, lakini kazi yake kuu ilikuwa kuhubiri kweli. (Luka 4:43; Yoh. 18:37; Mdo. 10:38) Aliwaamuru wafuasi wake ‘waende wakafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote na kuwafundisha.’ (Mt. 28:19, 20) Pia alisema kwamba wale wanaomwamini watafanya kazi hiyo aliyoianzisha kwa kiwango kikubwa zaidi. (Yoh. 14:12) Yesu aliiona kazi ya kuhubiri kuwa muhimu sana kwa sababu inawasaidia watu wajifunze njia ya wokovu.—Yoh. 17:3.
3 Mtume Paulo aliiona kazi yake ya kuhubiri kuwa “sharti,” yaani, takwa ambalo hakulipuuza. (1 Kor. 9:16, 17) Alikuwa tayari kujitoa kabisa, kuvumilia majaribu au magumu yoyote ili kutimiza huduma yake. (Mdo. 20:22-24) Mtume Petro na wenzake walionyesha roho hiyohiyo. Hata ingawa walifungwa na kupigwa, ‘waliendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.’—Mdo. 5:40-42.
4 Vipi sisi? Je tunaiona kazi hii ya kuhubiri habari njema ya Ufalme na kufanya wanafunzi kuwa jambo kuu maishani? Je, tunawahangaikia kwa moyo wale ambao ‘wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji’ kama vile Yesu alivyofanya? (Mt. 9:36) Matukio ya sasa na unabii wa Biblia unaonyesha wazi kwamba mwisho wa ulimwengu huu mwovu unakaribia! Tukikazia fikira umuhimu wa kazi ya kuhubiri tutatiwa moyo kuendelea kuhubiri kwa bidii.
5 Chunguza Hali Zako: Kwa kuwa hali za mtu hubadilika mara nyingi, inafaa kufikiria mara kwa mara ikiwa tunaweza kufanya marekebisho yoyote ili tushiriki zaidi katika kazi ya kuhubiri. Dada mmoja alikuwa painia wa kawaida katika miaka ya 1950, miaka ya 1960, na miaka ya 1970, lakini akalazimika kuacha kwa sababu ya ugonjwa. Hata hivyo, baada ya muda akapata nafuu. Hivi majuzi alichunguza tena hali zake na akaona kwamba anaweza kurudia upainia. Alifurahi kama nini kuhudhuria Shule ya Utumishi wa Painia akiwa na umri wa miaka 90! Vipi wewe? Je, unakaribia kustaafu au kuhitimu? Je, hali zako ambazo zimebadilika zinaweza kukuruhusu kuwa painia?
6 Yesu alipoona kwamba Martha amekengeushwa kwa ‘kushughulikia kazi nyingi,’ alimshauri kwa fadhili kwamba angepata baraka nyingi kwa kutoshughulikia mambo mengi. (Luka 10:40-42) Je, unaweza kupunguza shughuli zisizo za lazima katika maisha yako? Je, ni lazima wote wawili, yaani, mume na mke wafanye kazi? Je, mshahara wa mtu mmoja waweza kutosha mahitaji ya familia iwapo marekebisho fulani yanafanywa? Wengi wamenufaika kiroho kwa kufanya marekebisho fulani ili kushiriki zaidi katika huduma.
7 Sote na tufuate mfano wa Yesu na mitume wake! Bila shaka Yehova atabariki jitihada zetu za moyo wote tunaposhiriki tuwezavyo katika kazi muhimu ya kuhubiri habari njema za Ufalme.—Luka 9:57-62.