Yehova Ndiye wa Kusifiwa Sana
Mlo wa Jioni wa Bwana Utakaoadhimishwa Aprili 16
1 Tuna hamu kubwa tunapokaribia Aprili 16, 2003. Jioni hiyo tutajiunga na mamilioni ya waabudu wenzetu ulimwenguni pote kukumbuka kifo cha Yesu na kulisifu jina la Yehova. Yehova anastahili sifa zetu zote kwa sababu ya kutupatia zawadi ya kipekee ya fidia. Kupitia fidia hiyo, atawaletea wanadamu wote watiifu baraka za ajabu. Tunajiunga na mtunga-zaburi kwa moyo wote kuimba: “Bwana ndiye mkuu wa kusifiwa sana.”—Zab. 145:3.
2 Huo utakuwa wakati wa kutafakari wema wa Mungu na shukrani tunazopaswa kumpa Yehova kwa kututumia “Mwana wake mzaliwa-pekee kuingia katika ulimwengu ili tuweze kupata uhai kupitia kwake.” (1 Yoh. 4:9, 10) Tunapoadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana tunatambua kutoka mioyoni kwamba “BWANA ana fadhili, ni mwingi wa huruma . . . ni mwingi wa rehema.” (Zab. 145:8) Kwa kweli, fidia ndiyo njia kubwa zaidi ambayo Yehova ameonyesha upendo wake kwa wanadamu. (Yoh. 3:16) Tunapotafakari upendo wa Mungu na uaminifu wa Yesu, tunachochewa kumsifu Yehova. Tutamsifu milele kwa upendo wake mwingi sana wa kutuwezesha kupata uhai wa milele.—Zab. 145:1, 2.
3 Wasaidie Wengine Kumsifu Yehova: Tunapokaribisha wengine kujiunga nasi katika kumsifu Yehova tunaonyesha kwamba tunathamini zawadi kubwa zaidi ya fidia. Mtunga-zaburi aliongozwa na Mungu kuandika hivi: “Watalihubiri kumbukumbu la wema wako mkuu. Wataimba haki yako.” (Zab. 145:7) Mwaka jana pekee, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote walihubiri saa zaidi ya bilioni moja. Jitihada zao zilileta matokeo gani? Kwa wastani, zaidi ya watu 5,100 walibatizwa kila juma ili kuonyesha wakfu wao kwa Yehova. Kuna uwezekano mkubwa wa kupata ongezeko zaidi kwa kuwa watu 15,597,746 walihudhuria Ukumbusho. Idadi hiyo inatia ndani watu zaidi ya milioni 9 ambao bado hawajaanza kumsifu Yehova wakiwa watangazaji wa habari njema! Tukiwa watangazaji wa Ufalme, tunathamini pendeleo letu la kuhubiri habari njema na kuwaelekeza wengine upande wa Yehova, Mwana wake, na Ufalme wake.
4 Njia bora ya kuwatia moyo wengine kumheshimu Yehova ni kwa kuwakaribisha kujiunga nasi tunapoadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana. Je, umeandika orodha ya wale utakaoalika na vilevile wale utakaohitaji kuwakumbusha kuhusu siku na wakati? Je, umewaalika wote walio katika orodha yako? Iwapo bado, jitahidi kufanya hivyo katika muda unaobaki. Wasaidie waelewe kusudi la mwadhimisho huo. Kwenye mwadhimisho huo, uwe tayari kuwasalimia wageni. Wakaribishe kwa uchangamfu, wajulishe kwa wengine, na uwapongeze kwa kufika.
5 Kuhudhuria Ukumbusho kunaweza kuwachochea wapya wafanye maendeleo ya kiroho. Licha ya kwamba mwanafunzi mmoja ana tatizo la kuogopa kwenda mahali penye watu wengi kwa sababu alipatwa na tukio lenye kutisha, bado alihudhuria Ukumbusho. Alipoulizwa alionaje mkutano huo, alisema hivi: “Hiyo ilikuwa jioni ya pekee sana kwangu.” Tangu wakati huo, alianza kuhudhuria mikutano.
6 Baada ya Ukumbusho: Twawezaje kuwasaidia watu hao wenye kupendezwa wamsifu Yehova? Wazee watakuwa macho kutambua wageni watakaohudhuria Ukumbusho na kufanya mipango ili wahubiri wanaostahili wawatembelee bila kukawia na kuzungumzia mambo waliyojifunza na kujionea. Huenda wengine wakataka funzo la Biblia. Wanapaswa pia kualikwa kwenye mikutano yote ya kutaniko ya kila juma kwa kuwa wakihudhuria kwa ukawaida wataongeza ujuzi wao wa Biblia.
7 Mipango inafanywa ili kuwatia moyo wahubiri wote wasio wa kawaida na wasiotenda kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. Ukiombwa na wazee kumsaidia mhubiri asiyetenda kuanza tena kuhubiri tafadhali kubali mara moja. Kuwajali ndugu zetu kwa upendo kwa njia hiyo kunapatana na himizo hili la mtume Paulo: “Maadamu tuna wakati wenye kufaa kwa ajili ya hilo, acheni sisi tufanye lililo jema kuelekea wote, lakini hasa kuelekea wale ambao katika imani ni jamaa zetu.”—Gal. 6:10.
8 Sisi sote na tujitahidi kuhudhuria Ukumbusho Aprili 16. Hatungependa kukosa pindi hii ya pekee ya kumsifu Yehova. Naam, sasa na hata milele, acheni tumsifu Yehova kwa kazi zake kuu!—Zab. 145:21.