Iga Haki ya Yehova
1 “Yehova ni mpenda-haki.” (Zab. 37:28) Kwa hiyo, ingawa ameamuru kwamba ulimwengu huu usio mwadilifu uangamizwe, amefanya mpango ili onyo litangazwe kwanza. (Marko 13:10) Hatua hiyo huwapa watu nafasi ya kutubu na kuokolewa. (2 Pet. 3:9) Je, tunajitahidi kuiga haki ya Yehova? Je, taabu na mateso yanayowapata wanadamu hutuchochea kushiriki tumaini la Ufalme pamoja na wengine? (Met. 3:27) Kupenda haki kutatuchochea tushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri.
2 Hubiri Bila Ubaguzi: Tunapohubiri kusudi la Mungu kwa kila mtu bila kubagua, ‘tunatenda haki.’ (Mika 6:8) Lazima tupinge ule mtazamo usio mkamilifu wa kuwahukumu wengine kwa msingi wa kuonekana kwao. (Yak. 2:1-4, 9) “Mapenzi [ya Yehova] ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:4) Neno la Mungu la kweli linaweza kuleta mabadiliko makubwa katika maisha ya watu. (Ebr. 4:12) Kutambua jambo hilo kunaweza kutuchochea kuwafikia watu tukiwa na uhakika, hata wale ambao huenda walikataa kusikiliza hapo zamani.
3 Dada mmoja aliyekuwa akifanya kazi dukani alishtushwa na sura ya mteja mmoja wa kawaida. Hata hivyo, pindi inayofaa ilipofika, alijaribu kumhubiria mteja huyo kuhusu Paradiso ambayo Mungu ameahidi. Mwanamume huyo alijibu waziwazi kwamba haamini ngano na kwamba yeye ni mwasi wa utamaduni na hutumia dawa za kulevya. Lakini dada hakukata tamaa. Siku moja mwanamume huyo mwenye nywele ndefu alimwuliza dada maoni yake kuzihusu, kwa hiyo dada akamweleza maoni ya Biblia kuhusu nywele. (1 Kor. 11:14) Dada huyo alishangaa na kufurahi kwamba siku iliyofuata mwanamume huyo alikuwa amenyoa kinadhifu na alikuwa na nywele fupi! Mwanamume huyo aliomba funzo la Biblia, na ndugu mmoja akajitolea kumfundisha, kisha akaendelea hadi akajiweka wakfu na kubatizwa. Sawa na mwanamume huyo, wengi wanaomtumikia Yehova leo wanashukuru kwamba wale waliowaletea ujumbe wa Ufalme walifanya bidii yenye kuendelea bila kuonyesha ubaguzi.
4 Hivi karibuni Yehova ataondoa kabisa ukosefu wa uadilifu duniani. (2 Pet. 3:10, 13) Katika wakati huu mfupi unaobaki, na tuige haki ya Yehova kwa kuwapa wote nafasi ya kukimbia uharibifu unaokuja wa ulimwengu wa Shetani usio mwadilifu.—1 Yoh. 2:17.