Kampeni ya Pekee ya Kugawa Broshua Mpya
1 Watu wengi leo wanahangaishwa na hali za ulimwengu, lakini ni wachache wanaoelewa kwa nini hali ziko hivyo, jinsi wakati ujao utakavyokuwa, na kile wanachopaswa kufanya ili waokolewe katika hukumu inayokuja. (Eze. 9:4) Ili kuwasaidia watambue umuhimu wa nyakati zetu, kampeni ya pekee ya kugawa broshua mpya Endeleeni Kukesha! itafanywa kuanzia Jumatatu, Oktoba 18, hadi Jumapili, Novemba 14.
2 Broshua hiyo inaweza kutolewa katika huduma ya nyumba kwa nyumba, unapofanya ziara za kurudia, unapohubiri isivyo rasmi, au katika sehemu za umma. Hata hivyo, broshua Endeleeni Kukesha! haipaswi kutolewa kwa mtu yeyote tu. Badala yake, ni wale tu wanaoonyesha kwamba wanapendezwa na yale ambayo Biblia inasema kuhusu matukio ya ulimwengu ndio watakaoachiwa. Wale ambao hawapendezwi sana na ujumbe wetu, wanaweza kuachiwa trakti badala ya broshua.
3 Unaweza kuamsha upendezi wa mtu kwa kusema:
◼ “Watu wengi wanahangaishwa na matatizo makubwa na mambo yenye kuogofya yanayotokea sana leo. [Toa mfano wa kwenu.] Je, ulijua kwamba mambo hayo yalitabiriwa na Biblia? [Mruhusu ajibu. Kisha soma andiko linalofaa mfano uliotoa, kama vile Mathayo 24:3, 7, 8; Luka 21:7, 10, 11; au 2 Timotheo 3:1-5.] Biblia inaeleza umuhimu wa nyakati zetu na mambo yatakayowapata wanadamu wakati ujao. Je, ungependa kujua mengi zaidi? [Mruhusu ajibu. Mwachie broshua ikiwa kwa kweli anapendezwa.] Broshua hii inatolewa bila malipo. Ikiwa ungependa kutoa mchango kwa ajili ya kazi yetu ya ulimwenguni pote, tutafurahi kuukubali.”
4 Au huenda ukapendelea njia hii:
◼ “Watu wengi leo wanahangaishwa na matukio yenye kuogopesha au misiba inayowapata. Baadhi yao hujiuliza kwa nini Mungu haingilii kati na kukomesha mambo hayo. Biblia inatuhakikishia kwamba karibuni Mungu atachukua hatua ya kuwaondolea wanadamu mateso. Ona baraka ambazo Mungu atawaletea wanadamu. [Soma Zaburi 37:10, 11.] Je, ungependa kujua mengi zaidi?” Malizia kama ilivyoonyeshwa katika utoaji ulio hapo juu.
5 Jitahidi kujua jina la kila mtu anayekubali broshua na mahali anapoishi na upange kurudi ili kusitawisha upendezi ulioonyeshwa. Mapendekezo kuhusu njia za kufanya hivyo yatakuwa katika Huduma Yetu ya Ufalme ya Novemba 2004. Ikiwa mtu anapendezwa sana unapomtembelea katika ziara ya kwanza, unaweza kuanzisha funzo la Biblia mara moja ukitumia broshua Endeleeni Kukesha! au kichapo kingine kama vile broshua Anataka.
6 Nakala za broshua hiyo mpya zitapatikana katika Mkutano wa Utumishi ambao makala hii itazungumziwa. Inapendekezwa kwamba wahubiri na mapainia wachukue broshua watakazohitaji tu mwanzoni mwa kampeni hiyo. Yehova na abariki utendaji huu wa pekee kwa sifa yake na kwa faida ya watu wanyoofu kila mahali.—Zab. 90:17.