Uandalizi Mpya wa Kutusaidia Kujiepusha na Damu
Baraza Linaloongoza limeidhinisha kwamba mambo muhimu katika hati ya mamlaka ya kudumu ya uwakilishi (DPA) na kadi ya Mwelekezo wa Mapema Kuhusu Tiba/Ondoleo la Hatia yaunganishwe katika hati moja, ambayo mara nyingi itarejelewa kuwa kadi ya DPA.
Utahitaji kujaza kadi ya DPA kwa ajili ya nchi unayoishi. Kadi hiyo ya DPA itatumika kwa kuendelea nchini na pia kama taarifa ya kueleza mapendezi yako ya kitiba unaposafiri katika nchi nyingine. Wakati ujao itakubidi kujaza kadi mpya ya DPA ikiwa (1) utahitaji kufanya mabadiliko fulani kwenye kadi yako ya DPA, kama vile kubadili mapendezi yako, wawakilishi wako wa kitiba, anwani, na namba za simu, au (2) ikiwa kadi yako ya DPA imepotea au kuharibika.
Unapaswa kufikiria kwa sala na kujaza kadi ya DPA kwa uangalifu nyumbani. Lakini, kabla ya kutia sahihi, ni muhimu hatua zote za kisheria zifuatwe kikamili. Kwa mfano, ikiwa kadi yako inaonyesha kuwa mashahidi wawili wanapaswa kuona ukitia sahihi, wanapaswa wawepo unapoitia sahihi. Mara kwa mara waangalizi wa mafunzo ya kitabu wanapaswa kuwauliza wale ambao hawajajaza kadi mpya ikiwa wanahitaji msaada.
Kabla ya kuikunja kadi ya DPA, toa fotokopi nzuri kwa ajili ya mwakilishi wa kitiba, mwakilishi badala wa kitiba, na daktari na vilevile nakala moja kwa ajili ya rekodi zako. Huenda pia ukataka kutoa nakala nyingine kwa ajili ya washiriki wa familia yako na mwandishi wa kutaniko. Nakala hizo zinapaswa kuwa kwenye upande mmoja wa karatasi yenye ukubwa wa kawaida yaani, A-4, kadi ya DPA ikiwa katikati ya ukurasa huo. Unapaswa kubeba kadi yenyewe ya DPA si nakala yake.
Kitambulisho kilicho na tarehe 3/99 kwa ajili ya watoto ambao hawajabatizwa wa Mashahidi wa Yehova hakijabadilishwa. Wazazi wanapaswa kuhakikisha kadi ya mtoto imejazwa vizuri na kutiwa sahihi na kwamba kila mtoto awe ameibeba wakati unaofaa.
Wahubiri ambao hawajabatizwa wanaweza kutumia maneno ya kadi ya DPA na ya Kitambulisho ili kuandika maagizo ya kitiba kwa ajili yao na watoto wao. Mara tu mhubiri anapobatizwa, mwandishi anapaswa kumpa kadi ya DPA.