Sehemu ya 5: Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo
Kuamua Kiasi cha Habari Mtakachozungumzia
1 Alipowafundisha wanafunzi wake, Yesu alitilia maanani uwezo wao, kwa hiyo alizungumza nao “kwa kadiri walivyoweza kusikiliza.” (Marko 4:33; Yoh. 16:12) Katika njia hiyohiyo, walimu wa Neno la Mungu leo wanahitaji kuamua kiasi cha habari wanachoweza kuzungumzia kwenye funzo la Biblia. Hiyo itategemea uwezo na hali ya mwalimu na mwanafunzi.
2 Jenga Imani Thabiti: Huenda ukahitaji kutumia vipindi viwili au vitatu kujifunza sehemu fulani ili kuwasaidia baadhi ya wanafunzi waelewe sehemu hiyo, hali utahitaji kutumia kipindi kimoja tu na mwanafunzi mwingine. Kilicho muhimu si kujifunza habari nyingi katika muda mfupi, bali ni kumsaidia mwanafunzi aelewe vizuri mambo anayojifunza. Kila mwanafunzi anahitaji msingi imara wa imani yake mpya katika Neno la Mungu.—Met. 4:7; Rom. 12:2.
3 Unapoongoza funzo kila juma, tumia muda unaohitajika ili kumsaidia mwanafunzi aelewe na kukubali yale anayojifunza katika Neno la Mungu. Epuka kupitia haraka-haraka habari mnazozungumzia hivi kwamba mwanafunzi anakosa kunufaika kikamili na kweli anazojifunza. Mwe na wakati wa kutosha wa kukazia mambo makuu na kuzungumzia maandiko muhimu ambayo ndiyo msingi wa yale mnayojifunza.—2 Tim. 3:16, 17.
4 Usikengeushwe: Mbali na kuepuka kupitia haraka-haraka habari tunazozungumzia wakati wa funzo, tunahitaji kuepuka kuzungumzia mambo mengine yasiyohusiana na habari zile. Ikiwa mwanafunzi anapenda kuzungumzia sana mambo yake ya kibinafsi, huenda tukahitaji kupanga kuzungumzia mambo hayo baada ya funzo.—Mhu. 3:1.
5 Kwa upande mwingine, shauku yetu kuhusiana na kweli inaweza kufanya tuzungumze kupita kiasi wakati wa funzo. (Zab. 145:6, 7) Mara kwa mara, kutaja jambo lililoonwa au jambo lingine ili kuongezea yale mnayozungumzia kunaweza kumsaidia mwanafunzi, lakini hatungependa mambo hayo yawe mengi au marefu sana hivi kwamba mwanafunzi anakosa kuelewa kwa usahihi mafundisho ya msingi ya Biblia.
6 Kwa kuzungumzia kiasi kinachofaa cha habari kwenye kila funzo, tunawasaidia wanafunzi wa Biblia ‘watembee katika nuru ya Yehova.’—Isa. 2:5.