Sehemu ya 9—Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo
Kuwazoeza Wanafunzi Kutoa Ushahidi Isivyo Rasmi
1 Andrea na Filipo walipotambua kwamba Yesu ndiye Masihi aliyeahidiwa, hawakuweza kujizuia wasiwaambie wengine juu ya jambo hilo lenye kusisimua. (Yoh. 1:40-45) Vivyo hivyo leo, wanafunzi wa Biblia wanapoamini yale ambayo wanajifunza, wao husukumwa kusema kuyahusu. (2 Kor. 4:13) Tunawezaje kuwatia moyo watoe ushahidi isivyo rasmi na kuwazoeza kufanya hivyo kwa mafanikio?
2 Unaweza kumuuliza mwanafunzi ikiwa ameongea na wengine juu ya mambo ambayo amejifunza katika Biblia. Huenda ana marafiki au watu wa familia ambao anaweza kuwaalika kwenye funzo. Muulize ikiwa kuna yeyote ameonyesha upendezi kati ya wafanyakazi wenzake, wanafunzi wenzake, au watu wengine ambao anafahamiana nao. Kwa njia hiyo, anaweza kuanza kutoa ushahidi. Msaidie aelewe kwamba anahitaji kuwa na busara na kuonyesha heshima na fadhili anapoongea na wengine kumhusu Yehova Mungu na makusudi yake.—Kol. 4:6; 2 Tim. 2:24, 25.
3 Kuwahubiria Wengine: Ni muhimu sana kuwazoeza wanafunzi wa Biblia kutumia Neno la Mungu kuhubiri. Mnapofikia sehemu fulani za pekee katika funzo, muulize mwanafunzi maswali kama haya: “Wewe ungetumiaje Biblia kuwaeleza watu wa familia yenu kweli hii?” au “Ungetumia andiko gani katika Biblia kumthibitishia rafiki yako jambo hili?” Sikiliza jibu lake, na umwonyeshe jinsi anavyoweza kutumia Maandiko anapofundisha. (2 Tim. 2:15) Kwa kufanya hivyo, utakuwa ukimzoeza mwanafunzi kutoa ushahidi isivyo rasmi, na baadaye kuhubiri pamoja na kutaniko atakapostahili.
4 Ni jambo la hekima kuwasaidia wanafunzi wa Biblia kujua jinsi ya kushughulikia upinzani. (Mt. 10:36; Luka 8:13; 2 Tim. 3:12) Huenda wanafunzi wakapata fursa ya kutoa ushahidi wakati wengine wanapouliza maswali au wanapoongea kuwahusu Mashahidi wa Yehova. Broshua Mashahidi wa Yehova—Wao Ni Nani? Wanaamini Nini? inaweza kuwasaidia ili ‘wawe tayari kujitetea.’ (1 Pet. 3:15) Broshua hiyo ina habari sahihi ambazo wapya wanaweza kutumia kuwasaidia marafiki na watu wa familia wanaopinga wakiwa na nia nzuri waelewe imani yetu na utendaji wetu unaotegemea Biblia.