Sehemu ya 11—Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo
Kuwasaidia Wanafunzi Kufanya Ziara za Kurudia
1 Mwanafunzi wa Biblia anapoanza kuhubiri, atakutana na watu wanaopendezwa na habari njema. Tunawezaje kumsaidia mhubiri mpya afanye ziara za kurudia kwa njia nzuri na kuwasaidia watu wanaopendezwa?
2 Matayarisho kufanya ziara ya kurudia hufanywa katika ziara ya kwanza. Mtie moyo mwanafunzi apendezwe kikweli na wale anaowahubiria. (Flp. 2:4) Mzoeze hatua kwa hatua kuwatia moyo wanafunzi wajieleze, kusikiliza maelezo yao, na kutambua mambo yanayowahangaisha. Mtu akipendezwa, mwambie mhubiri huyo mpya aandike habari fulani muhimu kuhusu ziara hiyo. Tumia habari hiyo kumsaidia kujitayarisha kwa ajili ya ziara nyingine.
3 Kujitayarisha Kurudi: Pitia habari kuhusu ziara ya kwanza, na umwonyeshe mwanafunzi jinsi ya kuchagua ujumbe fulani kuhusu Ufalme ambao utamvutia mwenye nyumba. (1 Kor. 9:19-23) Tayarisheni pamoja utangulizi mfupi unaotia ndani andiko la Biblia na pia fungu moja katika kichapo cha funzo. Vilevile, tayarisheni swali linaloweza kuulizwa mwishoni mwa mazungumzo ili liwe msingi wa ziara itakayofuata. Mwonyeshe mhubiri huyo mpya jinsi ya kumfundisha mwenye nyumba jambo fulani kutoka katika Neno la Mungu kila mara anapomtembelea.
4 Ni vizuri pia kumzoeza mwanafunzi utangulizi mfupi wa ziara ya kurudia. Baada ya kumsalimu mwenye nyumba, anaweza kusema hivi: “Nilifurahia mazungumzo yetu ya wakati uliopita, na nimerudi ili tuzungumzie habari nyingine kutoka katika Biblia [taja habari hiyo].” Huenda ukahitaji pia kumwonyesha mhubiri huyo mpya jambo analoweza kufanya akimkuta mtu mwingine nyumbani.
5 Kufanya Ziara za Kurudia kwa Bidii: Mtie moyo mwanafunzi huyo aweke mfano mzuri kwa kuwarudia bila kukawia wote wanaopendezwa. Ili kuwapata watu nyumbani huenda tukahitaji kurudi tena na tena. Mfundishe mwanafunzi jinsi ya kupanga ziara za kurudia, na umsaidie kuelewa umuhimu wa kurudi kama anavyoahidi. (Mt. 5:37) Mzoeze mhubiri huyo mpya kuwa mwenye fadhili, mwenye kujali, na mwenye heshima anapowatafuta wale ambao ni mfano wa kondoo na kusitawisha upendezi wao.—Tito 3:2.