Sehemu ya 10—Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo
Kuwazoeza Wanafunzi Katika Huduma ya Nyumba kwa Nyumba
1 Wazee wanapoona kwamba mwanafunzi wa Biblia anastahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, mwanafunzi huyo anaweza kuanza kushiriki na kutaniko katika kazi ya kuhubiri hadharani. (Ona Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova, uku. 79-81.) Tunawezaje kumzoeza mwanafunzi kuhubiri nyumba kwa nyumba?
2 Kutayarisha Pamoja: Ni lazima ajitayarishe vizuri ili afaulu. Mwonyeshe mwanafunzi mahali ambapo anaweza kupata utangulizi katika Huduma Yetu ya Ufalme na kitabu Kutoa Sababu, na umsaidie kuchagua utangulizi rahisi ambao unafaa eneo lenu. Tangu mwanzo, mtie moyo atumie Biblia katika huduma yake.—2 Tim. 4:2.
3 Vipindi vya mazoezi humsaidia sana mhubiri mpya. Mwanafunzi anapojizoeza kutoa utangulizi, mwonyeshe jinsi ya kushughulikia kwa busara itikio la watu katika eneo lenu. (Kol. 4:6) Mhakikishie kwamba si lazima wahudumu Wakristo wajue jibu la kila swali ambalo huenda mwenye nyumba akauliza. Mara nyingi ni vizuri kumwambia mwenye nyumba kwamba ungependa kufanya utafiti kuhusu swali lake na utarudi baadaye kuzungumzia habari hiyo zaidi.—Met. 15:28.
4 Kuhubiri Pamoja: Mwanafunzi anaposhiriki kwa mara ya kwanza katika huduma ya nyumba kwa nyumba, mwache aangalie jinsi unavyotoa utangulizi ambao mlitayarisha pamoja. Halafu mshirikishe. Nyakati nyingine, huenda ikafaa kwa mwanafunzi huyo mpya kushiriki kidogo kwa kusoma andiko na kulifafanua. Zingatia utu na uwezo wa mwanafunzi. (Flp. 4:5) Mpongeze sana unapoendelea kumzoeza katika sehemu mbalimbali za kazi ya kuhubiri.
5 Ni muhimu kumsaidia mhubiri mpya kuwa na ratiba ya kushiriki kwa ukawaida katika huduma, na afanye hivyo kila juma ikiwezekana. (Flp. 3:16) Fanyeni mipango hususa ya kushiriki pamoja katika utumishi, na umtie moyo ahubiri pia na wahubiri wengine wenye bidii. Kielelezo chao na ushirika wao utamsaidia kuwa stadi na kupata shangwe katika mahubiri ya nyumba kwa nyumba.