Sehemu ya 12—Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo
Kuwasaidia Wanafunzi Kuanzisha na Kuongoza Mafunzo ya Biblia
1 Wanafunzi wetu wa Biblia wanapoanza kuhubiri huenda wakaogopa kuanzisha na kuongoza mafunzo yao ya Biblia. Tunaweza kuwasaidiaje wawe na maoni yanayofaa kuhusu sehemu hiyo muhimu ya huduma yetu?—Mt. 24:14; 28:19, 20.
2 Mwanafunzi wa Biblia anapostahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, yaelekea tayari yeye ni mwanafunzi katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Mazoezi anayopata anapotayarisha na kutoa hotuba anazopewa katika shule yatamsaidia kusitawisha sifa anazohitaji ili awe ‘mfanyakazi asiye na lolote la kuonea aibu, akilitumia sawasawa neno la kweli.’—2 Tim. 2:15.
3 Fundisha kwa Kuweka Mfano: Yesu aliwazoeza wanafunzi wake kwa kuwapa maagizo yaliyo wazi na kwa kuwawekea mfano bora. Alisema: “Kila mtu aliyefundishwa kikamili atakuwa kama mwalimu wake.” (Luka 6:40) Ni muhimu uige kielelezo cha Yesu kwa kuweka mfano mzuri katika huduma yako. Mwanafunzi anapoona mfano wako mzuri katika huduma, atatambua kwamba lengo la kufanya ziara za kurudia ni kuanzisha mafunzo ya Biblia.
4 Mweleze kwamba tunapomwalika mwenye nyumba ajifunze Biblia pamoja nasi, hatuhitaji kufafanua kwa undani jinsi funzo linavyoongozwa. Mara nyingi inafaa tu kumwonyesha jinsi funzo linavyofanywa kwa kujifunza naye fungu moja au mawili katika kichapo cha funzo. Mapendekezo yanayofaa ya kufanya hivyo yako kwenye ukurasa wa 8 wa nakala hii ya Huduma Yetu ya Ufalme na pia katika ukurasa wa 6 wa Huduma Yetu ya Ufalme ya Januari 2002.
5 Inapofaa, mwalike mwanafunzi aandamane nawe, au aandamane na mhubiri mwingine mwenye ustadi kwenye mafunzo mengine ya Biblia. Anaweza kutoa maelezo kuhusu fungu au andiko fulani la msingi. Hivyo, kwa kukutazama, mwanafunzi atajifunza mambo mengi kuhusu kuongoza mafunzo ya Biblia yenye maendeleo. (Met. 27:17; 2 Tim. 2:2) Mpongeze na umweleze jinsi anavyoweza kufanya maendeleo.
6 Kuwazoeza wahubiri wapya wawe walimu wa Neno la Mungu kutawawezesha kuwa na vifaa kamili kwa ajili ya “kazi njema” ya kuanzisha na kuongoza mafunzo yao wenyewe. (2 Tim. 3:17) Ni furaha iliyoje kufanya kazi bega kwa bega pamoja nao katika kutoa mwaliko huu wa upendo: “Yeyote anayetaka achukue maji ya uzima bure!”—Ufu. 22:17.