Sehemu ya 1: Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo
Funzo la Biblia Ni Nini?
1 Ulimwenguni pote, watu wa Mungu wanaongoza mafunzo ya Biblia yapatayo milioni sita kila mwezi. Kwa kutumia njia za kufundisha zenye matokeo, tunaweza kuwasaidia wanafunzi hao wa Biblia wafanye maendeleo hadi kufikia hatua ya kujiweka wakfu na kubatizwa na kuwa na “sifa za kustahili vya kutosha kufundisha wengine.” (2 Tim. 2:2) Je, ungependa kumsaidia mwanafunzi wako afanye maendeleo hayo? Kuanzia na toleo hili, Huduma Yetu ya Ufalme itakuwa na mfululizo wa makala zitakazoeleza mambo ya msingi ya kuongoza mafunzo ya Biblia yenye maendeleo.
2 Wakati wa Kuripoti Funzo la Biblia: Ikiwa unazungumza na mtu kwa ukawaida na kwa utaratibu kuhusu Biblia, hata ingawa ni kwa muda mfupi, ukitumia Biblia pamoja na kimoja cha vichapo vilivyopendekezwa, basi unaongoza funzo la Biblia. Hivyo ndivyo ilivyo hata ikiwa funzo linaongozewa mlangoni au kwa simu. Funzo hilo linaweza kuripotiwa wakati limeongozwa mara mbili baada ya kumwonyesha jinsi ya kujifunza na kama kuna sababu ya kuamini kwamba mtu huyo ataendelea kujifunza.
3 Broshua Anataka na kitabu Ujuzi ni vitabu vinavyotumiwa kuongoza mafunzo mengi ya Biblia. Baada ya kuvimaliza, ikiwa inaonekana kwamba mtu huyo anafanya maendeleo, hata kama ni polepole, na kwamba anasitawisha uthamini kwa yale anayojifunza, basi funzo hilo linaweza kuendelezwa katika kitabu Mwabudu Mungu. Broshua Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu! inaweza kutumiwa kujifunza na watu walio na elimu ndogo au uwezo mdogo wa kusoma.
4 Mafunzo ya Biblia yamekuwa na matokeo katika kuwasaidia mamilioni ya watu kuwa wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo. (Mt. 28:19, 20) Ukitumia madokezo yatakayotolewa katika makala zinazokuja za mfululizo huu, unaweza kuongoza funzo la Biblia lenye maendeleo.