Ongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo Mlangoni na kwa Kutumia Simu
1 Ni shangwe iliyoje kuanzisha funzo la Biblia! Hata hivyo, kumpata mtu anayependezwa kujifunza Biblia ni mwanzo tu. Kusudi la kuongoza funzo ni kumsaidia mtu awe mwanafunzi wa kweli wa Kristo. (Mt. 28:19, 20) Ni nini kinachoweza kutusaidia kutimiza mradi huo?
2 Watu Wenye Shughuli Nyingi: Leo watu wana shughuli nyingi. Katika sehemu fulani, huenda mwanzoni watu wengi wasipendezwe kutenga saa nzima kujifunza Biblia. Ili kuwasaidia watu hao, tumetiwa moyo kuanzisha na kuongoza mafunzo ya Biblia mlangoni au kwa kutumia simu. Mwanzoni, huenda mafunzo hayo yakaongozwa kwa muda mfupi na yakahusisha kuchunguza Maandiko machache tu ya Biblia kwa kutumia fungu moja au mawili ya kichapo kama vile Biblia Inafundisha. Ni jambo lenye kupendeza kama nini kwamba sasa wahubiri wengi wanaongoza mafunzo kama hayo mlangoni au kwa kutumia simu!
3 Hata hivyo, je, tunapaswa kuridhika kuendelea kuongoza funzo mlangoni? La. Ingawa ni jambo la hekima kutotumia muda mwingi sana tunapoongoza funzo kwa mara za kwanza, Huduma Yetu ya Ufalme ya Mei 1990 ukurasa wa 4 ilisema hivi: “Funzo likiisha kuimarishwa na upendezi wa mwenye nyumba kusitawishwa, kipindi kirefu zaidi cha wakati chaweza kutumiwa kwa funzo.” Jambo hilo ni muhimu. Kwa mfano: Huenda mwanzoni mtoto anayekaribia kufa kwa sababu ya njaa akalishwa kiasi kidogo cha chakula hadi apate tena hamu ya kula, lakini hatungetazamia apate tena nguvu kabisa au akue vizuri ikiwa angelishwa chakula kidogo hivyo miezi nenda miezi rudi. Vivyo hivyo, mwanafunzi wa Biblia anahitaji funzo rasmi na la kawaida ili awe mtumishi mkomavu wa Mungu.—Ebr. 5:13, 14.
4 Mafunzo ya Biblia Ndani ya Nyumba: Inapendekezwa funzo liongozwe mahali pa faragha kama vile ndani ya nyumba au mahali pengine panapofaa. Mahali kama hapo panaweza kufanya iwe rahisi zaidi kujifunza na kumsaidia mwanafunzi aelewe Neno la Mungu. (Mt. 13:23) Pia kufanya hivyo kutamwezesha mwalimu kupatanisha habari ya funzo na mahitaji ya mwanafunzi. Isitoshe, kuwa na kipindi kirefu zaidi cha funzo kutamwezesha mwanafunzi kuchunguza Neno la Mungu kabisa na kwa njia yenye kuimarisha imani.—Rom. 10:17.
5 Unaweza kubadilije mahali pa kufanyia funzo kutoka mlangoni hadi ndani ya nyumba? Baada ya kujifunza mara kadhaa kwa muda mfupi, kwa nini usimwombe mwenye nyumba mjifunze kwa kipindi kirefu zaidi? Au unaweza kutumia njia isiyo ya moja kwa moja kwa kumwuliza mtu huyo, “Je, unaweza kuwa na wakati leo wa kuketi tuzungumzie jambo hili pamoja?” au “Leo ungependa kutumia muda mrefu kadiri gani kuzungumzia jambo hili?” Ikiwa jitihada zako hazifaulu, endelea kuongoza funzo mlangoni kwa muda mfupi. Wakati mwingine unaofaa, jaribu tena kubadili funzo hilo liwe ndani ya nyumba.
6 Tunapoendelea kutafuta wale wanaostahili, na tusisahau kusudi letu la kuanzisha na kuongoza mafunzo ya Biblia. Mradi wetu ni kuwasaidia watu wenye moyo mnyoofu wawe watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu na kubatizwa. Tukiwa na lengo hilo, Yehova na abariki jitihada zetu tunapotimiza huduma yetu.—2 Tim. 4:5.
[Maswali ya Funzo]
1. Kusudi letu la kuongoza mafunzo ya Biblia ni nini?
2. Mafunzo ya Biblia mlangoni au kwa kutumia simu huongozwaje, na kwa nini yana matokeo?
3. Kwa nini tunapaswa kuongeza muda tunaotumia kuongoza funzo la Biblia mlangoni?
4. Kuna faida gani za kuongoza funzo la Biblia ndani ya nyumba?
5. Tunaweza kubadilije mahali pa kufanyia funzo kutoka mlangoni hadi ndani ya nyumba?
6. Tunapaswa kutimiza huduma yetu tukiwa na lengo gani, na mapendekezo katika makala hii yanaweza kutusaidiaje kulitimiza?