Kuwahubiria Watu Wengi Iwezekanavyo
1 Wanafunzi wa mapema wa Yesu walijitahidi sana kueneza ujumbe wa Ufalme. Walitumia njia zinazofaa ili kuwahubiria watu wengi iwezekanavyo habari njema. Waandikaji wa Biblia Wakristo, waliandika maandiko yao yaliyoongozwa kwa roho katika Kigiriki rahisi, ambacho wakati huo kilikuwa lugha ya kimataifa ya Milki ya Roma. Isitoshe, huenda wahubiri wenye bidii wa karne ya pili na ya tatu W.K. ndio walioitumia zaidi kodeksi, ambayo ilikuwa rahisi kutumiwa kutafuta andiko kuliko hati za kukunjwa.
2 Kutumia Teknolojia: Yehova alitabiri hivi kupitia nabii Isaya: “Kwa kweli utanyonya maziwa ya mataifa.” (Isa. 60:16) Katika utimizo wa siku zetu wa unabii huo, watumishi wa Yehova wanatumia mali za thamani kutoka kwa mataifa kuendeleza kazi ya kuhubiri. Kwa mfano, katika 1914, miaka mingi kabla biashara ya sinema zenye sauti haijasitawi, Wanafunzi wa Biblia walianza kuonyesha ile sinema yenye kichwa “Photo-Drama of Creation.” Slaidi na sinema hiyo yenye urefu wa saa nane, iliyo na picha zenye rangi na sauti, ilitumiwa kuwahubiria mamilioni ya watu.
3 Leo, watu wa Mungu wanatumia mashine zenye mwendo wa kasi sana na vifaa vinavyotumia kompyuta katika kuchapisha Biblia na vichapo vya Biblia katika lugha nyingi. Njia za haraka za usafiri hutumiwa kusafirisha vichapo vya Biblia hadi sehemu za mbali za dunia, na kuwafikia watu katika nchi 235. Yehova ametumia roho yake kuwachochea watumishi wake watumie teknolojia kama hiyo kwa njia nzuri, na hivyo kufanya kweli ya Biblia iwafikie watu wengi zaidi kuliko wakati mwingine wowote.
4 Marekebisho ya Kibinafsi: Waabudu wa kweli wamechochewa kufanya marekebisho ya kibinafsi ili waweze kuwahubiria habari njema watu wengi zaidi. Wengi wao wamerekebisha maisha yao ili washiriki zaidi katika kazi ya kuhubiri. Baadhi yao wamehamia maeneo yaliyo na uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Wengine wameongeza huduma yao kwa kujifunza lugha ya kigeni.
5 Tunaweza pia kuwahubiria watu wengi zaidi habari njema kwa kuhubiri wakati watu wanapopatikana nyumbani au kuhubiri mahali ambapo wanapatikana. Ikiwa katika eneo lenu mara nyingi watu hawapatikani nyumbani mchana, je, unaweza kubadili ratiba yako ili uhubiri jioni? Je, kuna maeneo ya umma ambayo unaweza kuhubiri? Je, umejaribu kuhubiri kwa simu au kuhubiri maeneo ya biashara? Je, wewe hutafuta fursa za kuhubiri isivyo rasmi?
6 Tuna pendeleo la pekee sana la kushiriki katika kazi kubwa ya kutangaza jina la Yehova na Ufalme wake! Acheni tuendelee kuwahubiria watu wengi iwezekanavyo kweli ya Neno la Mungu ambayo huleta uzima.
[Maswali ya Funzo]
1. Wakristo wa mapema walifanya nini ili waweze kuwahubiria watu wengi iwezekanavyo habari njema?
2, 3. (a) Andiko la Isaya 60:16 linatimizwaje leo? (b) Teknolojia inatumiwaje kuendeleza ibada safi?
4. Wahubiri fulani wamefanya marekebisho gani ili waweze kuwahubiria habari njema watu wengi zaidi?
5, 6. Tunaweza kufanya nini ili tuwahubirie watu wengi iwezekanavyo katika eneo letu?