Kuhubiri Kuhusu Ufalme Ni Pendeleo la Pekee
1 Kila siku, mabilioni ya watu duniani hunufaishwa na vitu vingi ambavyo Yehova huwaandalia ili waendelee kuwa hai. (Mt. 5:45) Hata hivyo, ni watu wachache sana walio na pendeleo la pekee la kumshukuru Muumba wao kwa kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. (Mt. 24:14) Unalithamini kadiri gani pendeleo hilo la pekee?
2 Kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme humletea Mungu heshima na huwapa tumaini na amani watu wanaosononeshwa na misukosuko ya leo. (Ebr. 13:15) Wale wanaoukubali ujumbe wa Ufalme watapata uzima wa milele. (Yoh. 17:3) Je, kuna kazi au taaluma yoyote katika ulimwengu inayoweza kutunufaisha jinsi hiyo? Mtume Paulo alitimiza huduma yake kwa njia iliyoonyesha kwamba aliithamini. Aliiona kuwa hazina.—Mdo. 20:20, 21, 24; 2 Kor. 4:1, 7.
3 Kulithamini Pendeleo Letu la Pekee: Njia moja ya kuonyesha kwamba tunalithamini pendeleo letu la kuhubiri ni kuzingatia ubora wa utumishi wetu. Je, tunajitahidi kutayarisha utangulizi ambao utagusa mioyo ya wasikilizaji wetu? Je, tunaweza kuboresha uwezo wetu wa kutumia Maandiko na wa kujadiliana na watu? Je, tunahubiri eneo letu kikamili? Je, tunaweza kuanzisha na kuongoza funzo la Biblia? Kama Wakristo waaminifu, wa nyakati zilizopita na wa siku hizi, sisi pia tunachochewa na mtazamo unaofaa kuelekea kazi hii, nasi tunalithamini sana pendeleo letu.—Mt. 25:14-23.
4 Ikiwa tunasumbuliwa na matatizo ya uzeeni, afya mbaya, au matatizo mengine, inafariji kujua kwamba jitihada na bidii yetu katika huduma inathaminiwa sana. Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba Yehova anathamini jitihada kama hizo za kumtumikia, kutia ndani jitihada ambazo huenda wengine wasizithamini.—Luka 21:1-4.
5 Kuhubiri kuhusu Ufalme huridhisha sana. Dada mwenye umri wa miaka 92 alisema hivi: “Ni pendeleo lililoje kufikiria miaka zaidi ya 80 ambayo nimekuwa nikimtumikia Mungu. Sina majuto yoyote! Ikiwa ningepewa nafasi nyingine, ningetumia maisha yangu kwa njia hiyohiyo kwa sababu, bila shaka, ‘fadhili zenye upendo za Mungu ni bora kuliko uzima.’” (Zab. 63:3) Sisi pia na tulithamini pendeleo hilo la pekee ambalo tumepewa na Mungu, yaani, pendeleo la kuhubiri kuhusu Ufalme.