Onyesha Unawajali Watu Kikweli—Kwa Kuwa Mwenye Utambuzi
1 Yehova Mungu na Kristo Yesu wana uwezo mkubwa wa kutambua mahitaji hususa ya watu na kuwasaidia. (2 Nya. 16:9; Marko 6:34) Tunapotambua mapendezi na mahangaiko ya watu tunaokutana nao katika huduma, tunaweza kubadili mazungumzo yetu kuhusu habari njema yafaane na hali zao.
2 Tambua Mambo Madogo-Madogo: Yesu alikuwa mwenye utambuzi. (Marko 12:41-43; Luka 19:1-6) Vivyo hivyo, tunapofika kwenye nyumba ya mtu na kuzingatia vitu tunavyoviona kama vile vitu vya watoto vya kuchezea, mapambo ya kidini, au maandishi yaliyobandikwa kwenye magari, itakuwa rahisi kuanzisha mazungumzo na kuhubiri habari njema kwa njia yenye matokeo.
3 Huenda sura na tabia ya mtu ikadhihirisha jambo fulani kuhusu hisia zake. (Met. 15:13) Labda amefiwa na mtu fulani ampendaye au amepatwa na hali fulani yenye kuhuzunisha na anahitaji kufarijiwa. Huenda mtu huyo akafurahi kusomewa maandiko fulani yanayofaa. (Met. 16:24) Je, mwenye nyumba anaharakisha kuondoka nyumbani au amemshika mtoto anayelia? Ikiwa ndivyo, huenda ikafaa kupanga kurudi wakati mwingine. Kwa kumjali mtu na ‘kumwonyesha hisia-mwenzi,’ huenda tukamchochea asikilize wakati tutakaporudi.—1 Pet. 3:8.
4 Badili Mazungumzo Yako Yafaane na Hali: Mtume Paulo alitambua kwamba jiji la Athene lilikuwa na madhabahu fulani iliyowekwa wakfu “Kwa Mungu Asiyejulikana.” Jambo hilo lilifanya abadili mazungumzo yake kuhusu habari njema, kwa kuwa alisema: “Kile mnachokipa ujitoaji-kimungu bila kujua, hicho ninawatangazia ninyi.” Njia hiyo ya busara ambayo Paulo alitumia iliwachochea baadhi ya wasikilizaji wake watafakari kuhusu ujumbe wa Ufalme na kuwa waamini.—Mdo. 17:23, 34.
5 Vivyo hivyo, kuwa wenye utambuzi hutusaidia kufahamu mapendezi ya mtu na hivyo kubadili mazungumzo yetu yamfae. Tumia maswali yanayoweza kumchochea mwenye nyumba ajieleze. Fikiria maandiko yanayoweza kutumiwa ili kumfanya apendezwe zaidi. (Met. 20:5) Kuwa wenye utambuzi na kuonyesha kwamba tunapendezwa kikweli na watu wengine, kutatusaidia kuhubiri habari njema kwa ustadi.