Onyesha Unawajali Watu Kikweli—Kwa Kubadilikana
1 Mtume Paulo aliweka mfano mzuri wa kubadili utoaji wake wa habari njema nyakati zote ili ufaane na malezi na kufikiri kwa wasikilizaji wake. (1 Kor. 9:19-23) Tunapaswa kujitahidi kufanya vivyo hivyo. Kwa kujitayarisha mapema, mara nyingi tunaweza kubadili mapendekezo yaliyo kwenye Huduma Yetu ya Ufalme ili yafae hali za watu katika eneo letu. Tunapokaribia mlango, tunaweza kutambua mambo yanayompendeza mwenye nyumba kisha tunaweza kutumia mambo hayo katika utoaji wetu. Hata hivyo, kuna njia nyingine tunayoweza kubadilikana katika utumishi wetu.
2 Badilikana Kulingana na Yale Watakayosema: Mara nyingi tunapohubiri habari njema, sisi huwauliza wenye nyumba swali na kuwaalika wajibu. Sisi huitikiaje jibu lao? Je, ni kawaida yako kuitikia kijuujuu tu na kuendelea na utoaji uliotayarisha? Au je, kile unachosema huonyesha kwamba unafikiria jibu la wenye nyumba? Unapoonyesha upendezi wa kweli kwa yale ambayo wengine wanasema, huenda ukatumia maswali mengine yenye busara ili kujua kile ambacho hasa wanafikiria. (Met. 20:5) Hivyo, unaweza kuzungumzia ujumbe wa Ufalme unaoshughulikia hasa mahangaiko ya msikilizaji.
3 Ili kufanya hivyo tunapaswa kuwa tayari kuzungumzia mambo mengine mbali na yale tuliyokuwa tumepangia. Tukianza kwa kuzungumzia tatizo lililotajwa katika vyombo vya habari naye mwenye nyumba ataje tatizo katika ujirani au jambo la kibinafsi linalomhangaisha, tamaa yetu ya kutosheleza mahitaji yake itatuchochea tubadili mazungumzo yetu ya Biblia ili yapatane na habari inayompendeza zaidi.—Flp. 2:4.
4 Kubadili Mazungumzo Yetu: Mwenye nyumba anapouliza swali, huenda ikafaa kuendeleza mazungumzo hayo wakati mwingine baada ya kutafuta habari za ziada kuhusu jambo hilo. Tunaweza pia kumtolea vichapo vinavyozungumzia jambo hilo kwa undani. Yote hayo yanaonyesha tunapendezwa kikweli kuwasaidia wengine wamjue Yehova.—2 Kor. 2:17.