Tunaweza Kusaidiaje?
1 Swali hili: “Tunaweza kusaidiaje?” huulizwa mara nyingi na Mashahidi wa Yehova wanaposikia kuhusu msiba ambao umetokea katika eneo fulani ulimwenguni. Andiko la Matendo 11:27-30 linaonyesha kwamba Wakristo katika karne ya kwanza walitoa msaada ili kuwasaidia ndugu zao waliokumbwa na njaa huko Yudea.
2 Katika nyakati zetu, sheria zinazohusu tengenezo letu zinaturuhusu kutumia fedha ili kuandaa msaada kwa ajili ya watu wanaokumbwa na misiba ya asili au ile inayosababishwa na wanadamu. Zinaturuhusu pia kutumia fedha hizo nyakati nyingine za uhitaji.
3 Kwa mfano, mwaka uliopita ndugu wengi walitoa msaada kwa ajili ya wale walioathiriwa na tsunami huko Asia Kusini. Hatua hiyo ya huruma ya kutoa michango ili kuandaa msaada inathaminiwa sana. Hata hivyo, kulingana na sheria za nchi fulani, michango inapotolewa kwa ajili ya msiba fulani mahususi, fedha hizo zinapaswa kutumiwa tu kwa kusudi ambalo mfadhili ametaja na katika kipindi fulani cha wakati, hata kama mahitaji ya ndugu zetu katika eneo linalohusika yamekwisha timizwa.
4 Kwa hiyo, inapendekezwa kwamba michango kwa ajili ya msaada iwekwe katika sanduku la michango ya kazi ya ulimwenguni pote. Hazina hiyo hutumiwa kutoa msaada na pia kushughulikia mahitaji ya kiroho ya ndugu zetu Wakristo. Ikiwa kwa sababu fulani mtu anataka kutoa mchango kwa kusudi tu la kuwasaidia akina ndugu, mchango wake utakubaliwa na kutumiwa kokote unakohitajiwa. Hata hivyo, ingefaa kama michango hiyo ingetolewa bila masharti ya jinsi itakavyotumiwa au mahali itakapotumiwa.
5 Tunapotoa michango yetu hasa kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote, tunakuwa na fedha zaidi za kutumia katika kazi zote zinazohusiana na Ufalme, badala ya kuhifadhi michango fulani kwa ajili tu ya kuandaa msaada wakati ujao. Hilo linapatana na andiko la Waefeso 4:16 linalotuhimiza tushirikiane kutoa kinachohitajiwa kwa ajili ya “ukuzi wa mwili ili huo ujijenge wenyewe katika upendo.”