Je, Wewe Huulizia Watu Wanaotaka Kujifunza?
Ikiwa kwa sasa unaongoza funzo la Biblia, kwa nini usimwulize mwanafunzi ikiwa rafiki zake na watu wa jamaa wangependa kujifunza mafundisho ya Biblia? Mara nyingi, mwanafunzi huyo atataja watu kadhaa. Baada ya kumwomba mwanafunzi huyo ruhusa, unaweza kutaja jina lake unapoenda kuwatembelea watu hao ili kuwauliza kama wangependa kujifunza Biblia. Huenda ukasema, “[Jina la mwanafunzi] amefurahia kujifunza Biblia, na anafikiri kwamba huenda wewe pia ukanufaishwa na programu yetu ya kufundisha watu Biblia bila malipo.” Kisha mwonyeshe kifupi jinsi ambavyo funzo huongozwa ukitumia kitabu Biblia Inafundisha.
Ikiwa una mwanafunzi ambaye anafanya maendeleo, unaweza kumtia moyo awaeleze rafiki zake na washiriki wa familia ambao huenda wakapendezwa, jinsi ambavyo sisi hujifunza Biblia na watu. Anaweza kuwaalika wahudhurie funzo lake. Au ikiwa haiwezekani, anaweza kupanga ukutane nao ili kuwaonyesha jinsi ambavyo funzo huongozwa. Kufanya hivyo kutamtia moyo mwanafunzi aanze kuwaeleza wengine habari anazojifunza kutoka katika Biblia.
Wale ambao wewe huwatembelea kwa ukawaida pia wanaweza kukutajia watu ambao wangependa kujifunza Biblia, hata ikiwa wao wenyewe hawajakubali kujifunza Biblia kwa ukawaida. Unapowaonyesha kitabu Biblia Inafundisha, huenda ukawauliza, “Je, unajua mtu yeyote ambaye angefurahia kupata kitabu hiki?”
Kwa kuzingatia uharaka wa nyakati tunamoishi, tungependa kutumia kila njia kuwasaidia watu wasikie na kukubali habari njema. Je, wewe huulizia watu wanaotaka kujifunza?