Onyesha Unawajali Watu Kikweli—Kwa Kuwapongeza
1 Pongezi ya kutoka moyoni huwatia watu moyo, huwachochea kutenda, na kuwaletea shangwe. Wahubiri wengi wameona kwamba, mara nyingi kuwapongeza wenye nyumba kutoka moyoni huwafanya wakubali kutusikiliza tunapowahubiria. Tunaweza kuwapongezaje watu tunapowahubiria habari njema?
2 Uwe Mtambuzi: Baada ya kurudi mbinguni, Yesu Kristo aliona matendo mazuri ya makutaniko kadhaa huko Asia Ndogo. (Ufu. 2:2, 3, 13, 19; 3:8) Vivyo hivyo, kuwajali kikweli watu tunaokutana nao shambani kutatufanya tutafute fursa za kuwapongeza. Kwa mfano, tunaweza kuwapongeza wengine tunapoona nyumba na uwanja wao ukiwa safi na nadhifu, tunapomwona mzazi akiwatendea watoto wake kwa upendo, au mwenye nyumba akitusalimu na kutukaribisha kwa urafiki. Je, wewe hutambua na kutumia fursa hizo?
3 Sikiliza kwa Makini: Unapowahubiria wengine, waombe watoe maoni yao kwa kuwauliza maswali yanayofaa. Waonyeshe heshima kwa kuwasikiliza kwa makini. (Rom. 12:10) Huenda mwenye nyumba akasema jambo ambalo unaweza kumpongeza kwa unyoofu na kuendeleza mazungumzo kwa kutaja jambo ambalo mnakubaliana.
4 Tumia Busara: Utafanya nini mwenye nyumba akisema jambo ambalo halipatani na kweli za Biblia? Badala ya kubishana naye, mshukuru kwa maoni yake, kisha uendeleze mazungumzo kwa kusema, “Naona kwamba umefikiria jambo hilo kwa uzito.” (Kol. 4:6) Hata kama mwenye nyumba ni mbishi, mara nyingi tunaweza kumpongeza kwa sababu amependezwa kikweli na habari tunayozungumzia. Huenda jibu hilo la upole likamtuliza mtu anayepinga sana habari njema.—Met. 25:15.
5 Ili pongezi iwe yenye kutia moyo, inapaswa kutoka moyoni. Usemi huo wenye kujenga humtukuza Yehova na huenda ukawavutia wengine wasikilize ujumbe wa Ufalme.