Tumwige ‘Mungu Wetu Mwenye Furaha,’ Yehova
1 Kwa kweli Yehova huwataka watu wawe na furaha. Neno lake hututia moyo tutarajie baraka za ajabu ambazo amekusudia kuwapa wanadamu. (Isa. 65:21-25) Inapaswa kuwa dhahiri kwa wote kwamba tunapata shangwe kwa kuwahubiria “habari njema yenye utukufu ya Mungu mwenye furaha.” (1 Tim. 1:11) Mazungumzo yetu kuhusu ujumbe wa Ufalme yanapaswa kuonyesha kwamba tunapenda kweli na tunawajali sana watu tunaowahubiria.—Rom. 1:14-16.
2 Ni kweli kwamba nyakati nyingine si rahisi kudumisha shangwe yetu. Katika maeneo fulani, ni watu wachache wanaokubali ujumbe wa Ufalme. Nyakati nyingine huenda tunakabili hali ngumu maishani mwetu. Ili tudumishe shangwe yetu, tunapaswa tutafakari kuhusu jinsi watu katika eneo letu wanavyohitaji kusikia na kuelewa habari njema ya Ufalme ambayo tunahubiri. (Rom. 10:13, 14, 17) Kutafakari jambo hilo kutatusaidia kuendelea kwa shangwe kuwajulisha watu kuhusu mpango wa rehema wa Yehova kwa ajili ya wokovu.
3 Zungumzia Mambo Mema: Pia tunahitaji kuzingatia yale tunayosema. Ingawa tunaweza kuanza mazungumzo kwa kutaja tatizo au habari fulani inayojulikana katika eneo, tunapaswa kuepuka kuzungumzia isivyo lazima mambo yenye kuvunja moyo. Tumepewa utume wa kuhubiri “habari njema za jambo bora.” (Isa. 52:7; Rom. 10:15) Habari hiyo njema ni ujumbe unaotegemea ahadi ya Mungu ya maisha mema ya wakati ujao. (2 Pet. 3:13) Kwa kuzingatia jambo hilo, tunapaswa kutumia Maandiko “kufunga majeraha ya waliovunjika moyo.” (Isa. 61:1, 2) Kufanya hivyo kutatusaidia sisi sote tudumishe shangwe na mtazamo mzuri.
4 Bila shaka, watu watatambua kwamba sisi ni wenye shangwe tunapohubiri. Hivyo basi, acheni nyakati zote, tumwige ‘Mungu wetu mwenye furaha,’ Yehova, tunapohubiri habari njema ya Ufalme katika eneo letu.