Twahubiri Habari Njema
1 Tuna pendeleo zuri ajabu la kuwa watangazaji wa “habari njema ya mambo mema!” (Rom. 10:15) Tuna ujumbe wenye kuburudisha wa kushiriki na watu wanaokabili msukosuko na kukata tumaini. Twaweza kuwasaidiaje watambue kwamba twawaletea “habari njema ya mambo mema”?—Isa. 52:7, italiki ni zetu.
2 Tayarisha Ujumbe Wenye Kujenga: Mazungumzo yetu hudumani yatakuwa na matokeo mazuri tukikazia mambo yenye kujenga. Kwa hiyo, tunapotayarisha utoaji wetu na kuchunguza kichapo tutakachotoa, twahitaji kukazia mambo yenye kujenga ya ujumbe huo. Tunapotoa tumaini letu linalotegemea Biblia kwa uhakika na kwa uchangamfu, twaweza kutazamia matokeo yenye kutia moyo.—Mit. 25:11.
3 Ijapokuwa twasikitika watu wanapoeleza jinsi ambavyo wameathiriwa na hali zinazoendelea kuharibika za ulimwengu, twapaswa kuwaeleza kwamba utatuzi halisi kwa matatizo ya mwanadamu ni Ufalme wa Mungu. Hata tunapozungumzia “siku ya kisasi,” ya Yehova, twataka kuonyesha jinsi mazungumzo hayo yamaanishavyo ‘habari njema kwa wanyenyekevu.’ (Isa. 61:1, 2) Twaweza kuwahakikishia wasikilizaji wetu kwamba kila kitu anachofanya Yehova mwishowe kitaleta furaha nyingi na matokeo mazuri zaidi.
4 Toa Kweli kwa Shangwe Halisi: Watu waonapo sura yetu yenye shangwe na sauti yetu yenye uhakika, wataelekea kutusikiliza. Tunapoonyesha mtazamo unaofaa, wasikilizaji wetu watafahamu kwamba ‘twashangilia katika tumaini.’ (Rom. 12:12) Wataelekea zaidi kukubali habari njema. Kwa hakika, tuna sababu nzuri sikuzote za kuonyesha mtazamo unaojenga, wenye shangwe katika kila sehemu ya huduma yetu.
5 Tukiwa wahudumu wa habari njema, sisi hufanya mengi zaidi ya kujulisha tu. Kuhubiri kwetu hutoa tumaini hakika la maisha bora sasa na vilevile wakati ujao. (1 Tim. 4:8) Tunapomfikia kila mtu, mtazamo wetu unaofaa wa akili utaonekana katika yale tunayosema na utasaidia watu wakubali habari njema. Kwa kukazia fikira yale tunayosema na jinsi tunavyoyasema, hebu na tuchochee watu wenye mioyo ya haki wakubali habari njema zenye kusisimua tunazohubiri!