‘Naweza Kufanya Nini?’
1 ‘Naweza kufanya nini?’ Bila shaka, swali hilo lilikuwa katika fikira za washiriki wa kikundi kidogo cha kujifunza Biblia kilichopangwa na Charles Taze Russell miaka ya 1870. Walipokuwa wakifanya maendeleo katika uelewevu wao wa mapenzi ya Mungu, wanafunzi hao wa mapema wa Biblia lazima wawe walijiuliza jambo ambalo wangeweza kufanya ili wasaidie wengine wajifunze kuhusu kusudi la Mungu. Ili kufikia ulimwengu mzima kwa ujuzi wa Biblia ambao walikuwa wakiupata, kwa kweli ilikuwa kazi kubwa sana.
2 Twafurahi kwamba walishughulikia tatizo hilo vizuri. Jinsi gani? Kila mtu alifanya sehemu yake iliyoonekana ndogo, hivi kwamba leo, Mashahidi wa Yehova wamejulikana ulimwenguni pote—tengenezo la karibu watangazaji wa Ufalme milioni sita, wakitumikia katika makutaniko 90,000 hivi katika nchi 234 na visiwa vya bahari!—Isa. 60:22.
3 Toa Tegemezo Lako Lote: Ni jambo muhimu kila mmoja wetu ashiriki katika kazi kubwa zaidi ambayo Yesu alitabiri ingefanywa siku hizi za mwisho. (Mr. 13:10) Hakika kazi hii haiwezi kuachiwa tu wazee wachache; wala kazi ya kuhubiri si ya kuachiwa mapainia tu. Kwa kweli, kila Mkristo aliyejiweka wakfu ana daraka la maana la kutimiza. Sisi sote twaweza kushiriki katika aina fulani ya utendaji wa kuhubiri. (1 Tim. 1:12) Tufanyapo hivyo kwa kadiri yoyote ile, twajinufaisha wenyewe na wengine.—1 Tim. 4:16.
4 Kila mmoja pia anaweza kutoa tegemezo lote kwa udugu wetu wa Kikristo katika njia nyingine za maana. Twaweza kutegemeza mikutano ya kutaniko kwa kuhudhuria kwa ukawaida na kwa kushiriki kwa uchangamfu. (Zab. 122:1, 8, 9) Twaweza kufanya sehemu yetu ili kuendeleza kutaniko likiwa safi kiadili. Twaweza kuandaa tegemezo la kifedha kwa kazi ya ulimwenguni pote, kulingana na uwezo wetu. Twaweza kushiriki kusafisha Jumba la Ufalme. Kila mtu anaweza kuchochea roho changamfu ya upendo na muungano katika kutaniko kwa kusaidia wapya, wachanga, na wazee vilevile.—Kol. 3:12, 14.
5 Kwa hiyo huenda ukauliza, ‘Naweza kufanya nini?’ Ijapokuwa jitihada zako za kibinafsi huenda zikaonekana kuwa ndogo, kwa kufanya sehemu yako, unachangia kutaniko lenye nguvu, lenye kutenda, na lililo na hali bora. Hivyo basi, sisi sote twaweza kuwa na fungu la maana katika kuheshimu jina la Yehova!