Tutatoa Toleo la Pekee la Amkeni! Mwezi wa Septemba
1 Karibu kila mtu hufurahia nyimbo za ndege na kushuka kwa jua. Hata hivyo, wengi hawakubali kwamba Baba wa mbinguni aliye na upendo ndiye aliyeumba vitu hivyo. Tutakuwa na nafasi ya pekee ya kutoa ushahidi kuhusu uumbaji wa Yehova kwa kusambaza toleo la pekee la Amkeni! (Isa. 40:28; 43:10) Toleo zima la Septemba litazungumzia kichwa hiki “Je, Kuna Muumba?”
2 Katika Eneo: Ikiwezekana, panga kuhubiri nyumba kwa nyumba pamoja na kutaniko kila Jumamosi. Bila shaka unaweza kutoa toleo hilo la pekee siku nyingine katika juma. Walimu na wengine wanaofanya kazi katika kitengo cha elimu watavutiwa sana na toleo hilo. Hivyo, mipango ya pekee inaweza kufanywa ili kuwatembelea watu kama hao wanaopatikana katika eneo lenu.
3 Mtu akipendezwa, muulize swali utakalojibu utakapomrudia. Kwa mfano, unaweza kumuuliza kuhusu sababu ambayo imemfanya Muumba mwenye upendo aruhusu watu wateseke sana. Kisha unapomrudia, unaweza kuzungumzia sura ya 1 au ya 11 ya kitabu Biblia Inafundisha. Au unaweza kumuuliza swali kuhusu kusudi la Muumba kwa dunia, kisha uzungumzie sura ya 3 unapomrudia.
4 Shuleni: Ukiwa shuleni, mbona usiwape walimu na wanafunzi wenzako toleo hilo la pekee la Amkeni! kama zawadi? Kuweka tu gazeti hilo juu ya dawati lako kunaweza kuwafanya wakuulize maswali kuhusu imani yako. Yaelekea utapata nafasi ya kutumia habari iliyo katika gazeti hilo unapoitetea imani yako darasani na unapoandika insha. Ili kukusaidia, toleo hilo lina makala “Vijana Huuliza” yenye kichwa “Ninaweza Kuiteteaje Imani Yangu Katika Uumbaji?”
5 Yehova anastahili heshima na utukufu kwa ajili ya vitu ambavyo ameumba. (Ufu. 4:11) Tunaweza kumheshimu Muumba wetu na kuwasaidia wengine wafanye hivyo kwa kutoa kwa bidii toleo la Septemba la Amkeni!