Wasaidie Wengine Wawe Marafiki wa Mungu
1 Leo, watu wa kila taifa wanafundishwa njia za Yehova. (Isa. 2:2, 3) Hata hivyo, ili wengine kama hao waweze “kuzaa matunda kwa uvumilivu,” lazima wampende Yehova. (Luka 8:15; Marko 12:30) Bila kuwa na upendo huo, hawatakuwa na nguvu za kukinza uvutano usiofaa au ujasiri wa kufanya yanayofaa. Njia moja ya kuwasaidia wengine kusitawisha uhusiano mzuri na Yehova ni kuwasaidia wakuze uthamini kwa sifa zake. Watie moyo wachunguze kwa makini habari iliyo katika kitabu Mkaribie Yehova.
2 Mfano Wako: Matendo yako yanaweza kuathiri sana mioyo ya wanafunzi wa Biblia. Wanapoona kwamba unathamini urafiki wako na Yehova na kuona jinsi urafiki huo unavyobadili maisha yako, huenda wakachochewa kusitawisha uhusiano kama huo. (Luka 6:40) Kwa kweli, mfano wetu huwa na uvutano mkubwa kwa wengine kuliko yale tunayosema.
3 Njia muhimu ambayo wazazi huwafundisha watoto wao kumpenda Yehova ni kupitia mfano wao. (Kum. 6:4-9) Wenzi fulani ambao walitaka kuwalea watoto wao katika kweli waliwaomba mashauri wazazi waliofanikiwa kufanya hivyo. Mume alisema, “Kila mtu niliyezungumza naye alisema kwamba jambo muhimu ni mfano wa wazazi.” Hivyo, katika kila sehemu ya maisha yao, wazazi wanaweza kuwawekea watoto mfano wa kinachomaanishwa na kuwa “rafiki ya Yehova.”—Yak. 2:23.
4 Sala ya Kutoka Moyoni: Unaweza kuwasaidia wengine pia kusitawisha urafiki na Yehova kwa kuwafundisha kusali kutoka moyoni. Unaweza kuwaonyesha sala ya mfano ya Yesu, kutia ndani sala nyingine nyingi za kutoka moyoni zilizo katika Maandiko. (Mt. 6:9, 10) Unaweza kuwafundisha watoto wako na wanafunzi wa Biblia jinsi ya kusali kupitia sala zako. Wanaposikia maneno yako ya kutoka moyoni, wanahisi jinsi wewe unavyohisi kumwelekea Yehova. Watie moyo ‘wadumu katika sala’ wanapokabili majaribu. (Rom. 12:12) Wakimwona Yehova akiwasaidia wanapokabili hali ngumu, watamtegemea na kumpenda kama rafiki wa kweli.—Zab. 34:8; Flp. 4:6, 7.