Je, Unaweza Kuingia Kwenye “Mlango Mkubwa Unaoongoza Kwenye Utendaji”?
1 “Mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji” ulipofunguliwa kwa mtume Paulo, alitumia nafasi hiyo kuendeleza kazi ya Ufalme kwa bidii licha ya kukabili wapinzani wengi. (1 Kor. 16:9) Leo, wahubiri wa Ufalme 642,000 ulimwenguni wameingia mlango huo mkubwa wa utendaji kwa kuwa mapainia wa kawaida.
2 Hali Hubadilika: Ingawa hali zetu za sasa za kibinafsi huenda zikatuzuia tusifanye mengi, hali hubadilika. Hivyo, ni vizuri tuchanganue hali zetu mara kwa mara badala ya kungoja hadi wakati ambapo hali zitatufaa kabisa. (Mhu. 11:4) Je, wewe ni kijana ambaye anakaribia kukamilisha masomo ya sekondari? Je, wewe ni mzazi ambaye ana watoto watakaoanza shule hivi karibuni? Je, unakaribia kustaafu? Huenda mabadiliko kama hayo yakatokeza nafasi na hivyo kukuwezesha kuanza upainia wa kawaida. Dada mmoja aliyekuwa na matatizo ya afya hapo awali, aliamua kujiandikisha kuwa painia akiwa na umri wa miaka 89. Kwa nini? Kwa vile hakuwa amelazwa hospitalini kwa zaidi ya mwaka mmoja, alihisi kwamba afya yake ingemruhusu kufanya upainia.
3 Katika kisa cha Paulo, mwanzoni alikusudia kuwatembelea ndugu zake huko Korintho. Hata hivyo, alifanya marekebisho fulani kwa ajili ya habari njema. Wengi ambao ni mapainia wa kawaida leo walihitaji kufanya mabadiliko fulani ili wafanye upainia. Wengine wamerahisisha maisha yao hivi kwamba wanahitaji tu kufanya kazi ya muda ili kujiruzuku kwa sababu gharama zao zimepungua. Wanafurahia pendeleo lao la utumishi. (1 Tim. 6:6-8) Wenzi fulani wa ndoa wamefanya mabadiliko ili mume afanye kazi ya kuajiriwa na kumruhusu mke kufanya upainia.
4 Usifanye haraka kukata kauli kwamba huwezi kufanya upainia kwa sababu huna uhakika iwapo utatimiza takwa la saa. Unahitaji tu kufanya saa mbili hivi kila siku. Ikiwa huna uhakika, jaribu kufanya upainia msaidizi kwa mwezi mmoja au miwili lakini ukiwa na mradi wa pekee wa kutimiza saa 70. Hilo litakuwezesha kuonja shangwe ya upainia. (Zab. 34:8) Zungumza na mapainia. Huenda walishinda vizuizi kama vyako. (Met. 15:22) Mwombe Yehova abariki jitihada zako za kupanua utumishi wako.—1 Yoh. 5:14.
5 Mradi Wenye Faida: Kufanya upainia wa kawaida huleta baraka nyingi. Unakuruhusu kupata furaha nyingi inayotokana na kutoa zaidi. (Mdo. 20:35) Upainia utaboresha uwezo wako wa kutumia sawasawa Neno la Mungu la kweli. (2 Tim. 2:15) Utakuwa na nafasi nyingi za kuona mkono wa Yehova ukifanya kazi kwa niaba yako. (Mdo. 11:21; Flp. 4:11-13) Pia, upainia utakusaidia kukuza sifa za kiroho, kama vile uvumilivu, na utakuwezesha kumkaribia Yehova zaidi. (Yak. 4:8) Je, unaweza kuingia mlango huu mkubwa wa utendaji na kuwa painia wa kawaida?
[Maswali ya Funzo]
1. Ni ‘mlango gani mkubwa unaoongoza kwenye utendaji’ ambao umefunguliwa kwetu?
2. Kwa nini ni vizuri kuchanganua hali zetu mara kwa mara?
3. Wengine wamefanya marekebisho gani ili wawe mapainia wa kawaida?
4. Tunaweza kufanya nini ikiwa hatuna uhakika kwamba tutatimiza takwa la saa?
5. Kwa nini upainia wa kawaida ni mradi wenye faida?