Sasa Ndio Wakati wa Kuhubiri!
1 “Mwogopeni Mungu na kumpa utukufu.” Malaika anaelekeza kazi ya kutangaza ujumbe huo “kwa kila taifa na kabila na lugha na watu.” Kwa nini? “Kwa sababu saa ya hukumu ya [Mungu] imefika.” Leo tunaishi katika hiyo “saa ya hukumu,” ambayo itafikia upeo mfumo huu wa mambo utakapoharibiwa. Ni muhimu watu ‘wamwabudu Yeye aliyezifanya mbingu na dunia na bahari na chemchemi za maji.’ Hakuna kazi nyingine yoyote iliyo muhimu na inayopaswa kufanywa haraka kuliko kazi ya kutangaza “habari njema ya milele.” Naam, sasa ndio wakati wa kuhubiri!—Ufu. 14:6, 7.
2 Katika miaka kumi iliyopita, watumishi wa Yehova wametumia karibu saa bilioni 12 kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Wengi wao wamefanya marekebisho maishani ili washiriki zaidi katika mavuno ya kiroho. (Mt. 9:37, 38) Kwa mfano, mwaka jana, zaidi ya wahubiri 850,000 kwa wastani walikuwa mapainia. Kila mwezi, mapainia wa kawaida wanapaswa kuhubiri saa 70 kwa wastani. Mapainia wasaidizi wanapaswa kuhubiri saa 50.
3 Unachohitaji Kufanya Ili Uwe Painia: Mapainia hujitahidi kuishi maisha sahili kwa kuwa wanatambua kwamba “wakati uliobaki umepungua.” (1 Kor. 7:29, 31) Wao hutafuta njia za kupunguza gharama zao ili wasitumie wakati mwingi kufanya kazi ya kimwili. Kwa mfano, baadhi yao wamehamia nyumba ndogo. Wengine wameachana na vitu wasivyohitaji. (Mt. 6:19-21) Nyakati nyingine wamelazimika kupunguza shughuli zao za kibinafsi. Wanafanya yote hayo ili wawe na wakati mwingi zaidi wa kushiriki katika huduma. (Efe. 5:15, 16) Kwa kuendelea kujitahidi, kuonyesha roho ya kujidhabihu, na kwa kumwomba Yehova awategemeze, wahubiri wengi wamefanikiwa kuwa na ratiba nzuri ambayo imewawezesha kutumikia wakiwa mapainia.
4 Unaweza kuwa painia? Waombe mapainia wenye mafanikio wakueleze jinsi wanavyotimiza huduma yao. Hubiri pamoja nao na upate shangwe kama wao. Soma makala zinazohusu upainia katika vichapo vyetu. Jiwekee miradi inayofaa maishani mwako ambayo hatimaye itakuwezesha kuwa painia. Iwapo huwezi kwa sasa kuwa painia kwa sababu ya matatizo fulani, unaposali, mweleze Yehova kuyahusu na umwombe akusaidie kuyatatua.—Met. 16:3.
5 Baraka na Shangwe: Upainia huboresha uwezo wetu wa kutumia Neno la Mungu, na hilo hutuletea shangwe nyingi. Dada fulani kijana ambaye ni painia alisema kwamba “inanufaisha sana kuweza kulitumia sawasawa Neno la Mungu la kweli. Unapokuwa painia unatumia Biblia mara nyingi sana. Sasa ninapohubiri mlango kwa mlango ninaweza kukumbuka maandiko yanayomfaa kila mwenye nyumba.”—2 Tim. 2:15.
6 Pia upainia humfunza mtu mambo mengi yaliyo muhimu maishani. Unaweza kuwasaidia vijana wajue jinsi ya kutumia wakati kwa hekima, kupangia matumizi ya pesa, na jinsi ya kuishi na wengine kwa amani. Upainia umewawezesha wengi wasitawishe maoni ya kiroho maishani. (Efe. 4:13) Isitoshe, mapainia hufurahia pendeleo la pekee la kusaidiwa na kubarikiwa na Yehova.—Mdo. 11:21; Flp. 4:11-13.
7 Mojawapo ya faida kubwa zaidi za kuwa painia ni kwamba upainia hutusaidia kumkaribia Yehova. Hilo linaweza kutuimarisha tunapokabili majaribu. Dada fulani aliyevumilia hali ngumu sana alisema hivi: “Uhusiano wa karibu pamoja na Yehova, ambao nimesitawisha nikiwa painia, ulinisaidia kukabili hali hiyo ngumu.” Aliongeza hivi: “Ninafurahi sana kwamba nimetumia maisha yangu kumtumikia Yehova wakati wote. Nimeweza kumtumikia kwa njia mbalimbali ambazo sikudhani ningeweza.” (Mdo. 20:35) Sisi pia na tupate baraka tele tufanyapo yote tunayoweza katika kazi hiyo ya kuhubiri, ambayo ndiyo kazi muhimu zaidi.—Met. 10:22.
[Maswali ya Funzo]
1. Kwa nini sasa ndio wakati wa kuhubiri?
2. Watumishi wa Yehova wanaonyeshaje kwamba wanatambua uharaka wa nyakati tunamoishi?
3. Wahubiri wanahitaji kufanya marekebisho gani ili wawe mapainia?
4. Unaweza kufanya nini ili ufikie mradi wa kuwa painia?
5. Upainia unatusaidiaje kuboresha uwezo wetu wa kuhubiri?
6. Upainia humfunza mtu mambo gani?
7. Upainia unatusaidiaje kumkaribia Yehova?