Sanduku La Swali
◼ Kuna hatari gani za kuwasiliana na mtu tusiyemfahamu kwenye Intaneti?
Vituo vingi vya kuwasiliana kwenye Intaneti vimebuniwa ili watu waweze kuwasiliana na kufahamiana. Vingi kati ya hivyo huwaruhusu watu kutengeneza na kuweka mambo yao, ambayo yanaweza kutia ndani picha na habari nyingine za kibinafsi. Watu wanapoona maelezo hayo wanaweza kuanza kuwasiliana na wenye habari hizo. Vituo kama hivyo ni maarufu sana miongoni mwa vijana, na vijana wengine katika kutaniko wamevitumia kuwasiliana na watu wengine ambao wanadai kuwa Mashahidi wa Yehova.
Ni rahisi kwa mtu tunayewasiliana naye kupitia Intaneti kutudanganya kuhusu yeye ni nani, hali yake ya kiroho, au malengo yake. (Zab. 26:4) Mtu anayedai kuwa Shahidi wa Yehova anaweza kuwa mtu asiyeamini, mtu aliyetengwa na ushirika, au hata mwasi-imani. (Gal. 2:4) Imeripotiwa kwamba, watu wengi wanaopenda kufanya ngono na watoto wanatumia vituo hivyo kupata mawindo yao.
Hata kama tuna hakika kabisa kwamba watu tunaowasiliana nao wana msimamo mzuri kutanikoni, mazungumzo katika hali kama hiyo yanaweza kwa urahisi kubadilika na kuwa mazungumzo yasiyofaa. Kwa sababu kwa kawaida watu hujihisi huru sana wanapowasiliana na watu ambao hawajakutana nao ana kwa ana. Wanaweza pia kuona kuwasiliana kupitia Intaneti kama faragha na kufikiri kwamba chochote wanachosema hakitajulikana na watu wengine, kama vile wazazi wao au wazee. Kwa kusikitisha vijana fulani wanaotoka katika nyumba za Kikristo wamenaswa na kuhusika katika mazungumzo machafu. (Efe. 5:3, 4; Kol. 3:8) Wengine wameweka picha zao zenye kuamsha hamu ya ngono, majina machafu ya utani, au wameweka miziki yenye maneno machafu ya kingono kwenye vituo vyao.
Kutokana na mambo yaliyoelezwa hapo juu, wazazi wanapaswa kufuatilia kwa makini watoto wao wanafanya nini kwenye intaneti. (Met. 29:15) Ni hatari kualika mtu tusiyemjua nyumbani mwetu au kumruhusu awe peke yake na watoto wetu. Vivyo hivyo, ni hatari kwetu au kwa watoto wetu kuanzisha urafiki na watu tusiowajua kwenye Intaneti, hata kama wanadai kuwa ni Mashahidi wa Yehova.—Met. 22:3.