Fuata Kielelezo Kilichowekwa na Yesu
1 Tunaposhiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi, tunapaswa kukumbuka kwamba kielelezo chetu kinaweza kuwaathiri sana watu wanaotutazama. Yesu alifundisha kwa maneno na vitendo. Wale waliokuwa wakimtazama wangeweza kuona bidii yake, upendo wake kuelekea watu, hamu yake ya kutakasa jina la Baba yake, na azimio lake la kutimiza mapenzi ya Baba yake.—1 Pet. 2:21.
2 Tunapohubiri Nyumba kwa Nyumba: Kama Yesu, kielelezo chetu kinaweza kuwachochea wale wanaohubiri pamoja nasi. Wapya na wahubiri wasio na uzoefu ambao wanatuona tukishiriki kwa bidii katika huduma, wanaweza kufikiria jinsi wanavyoweza kuboresha utumishi wao. Wanapoona shangwe yetu na jinsi tunavyopendezwa na watu, watakumbushwa umuhimu wa kuonyesha sifa hizo wanapohubiri. Wanapoona jinsi tunavyotumia Maandiko, tunavyofanya ziara za kurudia, na kuongoza mafunzo ya Biblia, watatiwa moyo kufanya vivyo hivyo.
3 Tunapoongoza Mafunzo ya Biblia: Wanafunzi wetu wa Biblia wataangalia mwenendo wetu. Kwa mfano, ingawa tunaweza kuwaeleza umuhimu wa kujiandaa kwa ajili ya funzo, kuchunguza maandiko, na kupigia majibu mstari, watachunguza ikiwa sisi tumefanya hivyo. (Rom. 2:21) Ikiwa tunafika kwa wakati kulingana na jinsi tulivyoahidiana nao, hawataruhusu chochote kivuruge funzo lao la Biblia. Bila shaka, wataona pia jinsi tunavyojidhabihu katika huduma na imani yetu yenye nguvu. Haishangazi kwamba wanafunzi wa wale ambao hufuata kwa ukaribu kielelezo cha Yesu wanakuwa wenye bidii, na kufanikiwa katika mahubiri.
4 Tunapohudhuria Mikutano ya Kutaniko: Wale wote ambao wako katika kutaniko la Kikristo wana nafasi ya kufundisha kupitia vielelezo vyao kwenye mikutano. Watu wanaopendezwa wanapoanza kuhudhuria mikutano wanafaidika kutokana na kielelezo wanachokiona kutanikoni. Wataona undugu wetu mchangamfu, umoja wetu wa Kikristo, na kuvaa na kujipamba kwetu kwa kiasi. (Zab. 133:1) Watashuhudia jinsi tunavyohudhuria kwa uaminifu mikutano na jinsi tunavyotoa tangazo la hadharani la imani yetu. Mgeni mmoja alipohudhuria mkutano, alishangazwa na jinsi binti mdogo alivyoweza kupata haraka andiko katika Biblia yake na jinsi alivyokuwa akifuatana na msomaji kwa makini. Kielelezo cha binti huyo kilimchochea mgeni yule kuomba funzo la Biblia.
5 Maandiko hutuhimiza tujifunze kutokana na vielelezo vizuri vya waamini wenzetu. (Flp. 3:17; Ebr. 13:7) Kwa hiyo, tunapaswa kukumbuka kwamba ikiwa tunafuata kwa makini kielelezo kilichowekwa na Yesu, wengine wataona na kuchochewa. Tukitambua hilo, acheni tukumbuke maneno yanayopatikana katika 1 Timotheo 4:16: “Jiangalie daima wewe mwenyewe na kufundisha kwako.”
[Maswali ya Funzo]
1. Yesu aliweka kielelezo gani?
2. Ni katika njia zipi kielelezo chetu kinaweza kuwaathiri wale tunaohubiri nao?
3. Kielelezo chetu kinaweza kuwasaidiaje wanafunzi wa Biblia, na wanaweza kujifunza nini?
4. Tunapohudhuria mikutano mfano wetu unawafundisha wengine nini?
5. Kwa nini hatupaswi kupuuza thamani ya kielelezo chetu?