Usiwanyime Watu Mema!
1 Kwa kushiriki kikamili katika kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu, ‘hatuwanyimi mema’ watu walio katika eneo letu. (Met. 3:27) Hakuna ujumbe ulio bora zaidi tunaoweza kushiriki na wanadamu kuliko kuwaambia kuhusu hali njema zitakazokuwapo chini ya utawala wa Mungu. Ingawa huenda unahubiri sana kwa njia isiyo rasmi kuhusu tumaini la Ufalme au kuwaachia watu vichapo, ikiwa huongozi funzo la Biblia, kwa nini usiwe na mradi wa kufanya hivyo?
2 Nyakati nyingine huenda hisia zetu kuhusu kuongoza mafunzo ya Biblia zikawa kizuizi. Wengine wanasita kuongoza funzo la Biblia kwa sababu wanahisi hawastahili au kwa sababu ya ratiba yenye shughuli nyingi. Mapendekezo yafuatayo yanaweza kukusaidia usisite kuongoza mafunzo ya Biblia.—Mt. 28:19; Mdo. 20:20.
3 Kuhisi Hustahili: Huenda huna elimu ya kutosha au kwa sababu fulani unahisi huna ustadi wa kuongoza funzo la Biblia. Wahudumu Wakristo wenye matokeo katika karne ya kwanza walikuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu.” Ni nini kilichowawezesha kuwafundisha wengine kweli? “Walikuwa pamoja na Yesu.” (Mdo. 4:13) Walijifunza kutoka kwa Mwalimu Mkuu, Yesu, ambaye mafundisho na njia yake ya kuhubiri imerekodiwa katika Maandiko kwa ajili yetu. Hata iwe huna elimu ya kutosha, unapata elimu ya kiroho ambayo haiwezi kulinganishwa na elimu nyingine.—Isa. 50:4; 2 Kor. 3:5.
4 Mara nyingine Yehova aliwatumia manabii kuwarekebisha watawala au watu wengine wenye vyeo waliokosea. Wengine, kama vile Amosi, walikuwa watu wa hali ya chini. Amosi alikiri hivi: “Mimi sikuwa nabii, wala sikuwa mwana wa nabii, bali nilikuwa mchungaji na mminyaji wa tini za mikuyu.” (Amo. 7:14) Hata hivyo, Amosi hakusita kufikisha ujumbe wa hukumu za Yehova kwa Amazia, kuhani aliyeabudu ndama. (Amo. 7:16, 17) Nyakati zote tunapaswa kukumbuka kwamba tunafanya kazi ya Mungu, naye atatupa sifa za kustahili vya kutosha kutekeleza kazi hiyo.—2 Tim. 3:17.
5 Ratiba Yenye Shughuli Nyingi: Ingawa una ratiba yenye shughuli nyingi, inaelekea kwamba tayari umetenga wakati wa kushiriki kwa kawaida katika utumishi. Kuongoza funzo la Biblia kunaweza kuwa sehemu yenye kufurahisha sana ya utumishi. Ni pendeleo kuona Neno la Yehova likibadili maisha ya mtu. (Ebr. 4:12) Yehova anafurahi tunapojidhabihu ili kumsaidia mtu ‘apate ujuzi sahihi wa kweli.’ (1 Tim. 2:4) Hata malaika wanashangilia wakati mtu anapotubu na kuacha maisha yake ya awali, na kufanya maendeleo ya kiroho.—Luka 15:10.
6 “Mapenzi [ya Mungu] ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:4) Tuna pendeleo kubwa kama nini la kutenda kupatana na mapenzi ya Mungu! Ili tufanye hivyo, hatupaswi kusita kuongoza mafunzo ya Biblia.
[Maswali ya Funzo]
1. Ni katika njia gani ‘hatuwanyimi watu mema’?
2. Ni nini kinachoweza kutufanya tusite kuanzisha funzo la Biblia?
3. Kwa nini tuna sifa za kustahili kuwafundisha watu Biblia?
4. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Amosi?
5. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kuanzisha funzo la Biblia hata ikiwa tuna ratiba yenye shughuli nyingi?
6. Tuna pendeleo gani katika kutimiza mapenzi ya Mungu?