Hubiri Bila Kuacha
1 Huenda nyakati nyingine tukahisi kwamba eneo letu limehubiriwa kikamili zaidi na mara kwa mara lakini watu wengi hawakubali ujumbe wetu. Hata hivyo, tuna sababu nzuri sana za kuendelea kuhubiri.—Mt. 28:19, 20.
2 Kuwa Ushahidi: Yesu alitabiri kwamba kazi ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme ingekuwa sehemu muhimu sana ya ile ishara yenye matukio mengi ya “umalizio wa mfumo wa mambo” na kwamba kazi hiyo ingefanywa “ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mt. 24:3, 14) Watu wanapotuona tukihubiri habari njema ya Ufalme, wanapata ushahidi mkubwa sana. Baada ya kuondoka kwenye eneo, huenda watu fulani wakazungumza kuhusu ziara yetu kwa saa nyingi au kwa siku nyingi, hata ikiwa hawakusikiliza ujumbe wetu. Kuthamini umuhimu wa huduma yetu kunatusaidia kuendelea kuhubiri tujapokabili upinzani. Tunampendeza Yehova tunaposhiriki kutimiza unabii wa Biblia kwa kutoa ushahidi na kuwaonya watu.—2 The. 1:6-9.
3 Ustahimilivu Unahitajiwa: Kwa kuwa watu wanakengeushwa fikira na mambo mengi sana na wana shughuli nyingi sana, tunahitaji kuwa wastahimilivu tunapojitahidi kuwachochea wapendezwe na ujumbe wetu. Mwanamke mmoja alitembelewa kila juma kwa mwaka mmoja na Shahidi fulani kabla ya kuamua kumkaribisha Shahidi huyo nyumbani mwake ili wazungumzie Biblia. Alifurahia sana mambo aliyosikia hivi kwamba alikubali kujifunza Biblia, akaanza kuhudhuria mikutano, na muda si muda akaamua kubatizwa.
4 Hali za ulimwengu zinabadilika haraka sana, ndivyo na mitazamo ya watu. Watu wengi waliokataa tusiwatembelee zamani, huenda sasa wakakubali ujumbe tunaotangaza ambao unaburudisha na kuwapa watu tumaini. Hata mtu mmoja tu akikubali ujumbe wa Ufalme, ustahimilivu wetu utakuwa umezaa matunda.
5 Watu wengi zaidi na zaidi ulimwenguni pote ‘wanaugua na kulia kwa sababu ya machukizo yote yanayofanywa.’ (Eze. 9:4) Matokeo ya kazi yetu ya kuhubiri Ufalme yanathibitisha kwamba watu wenye mwelekeo wa uadilifu wanakubali ujumbe wa Ufalme. (Isa. 2:2, 3) Kwa hiyo, acheni tuendelee kuhubiri bila kuacha na kustahimili kwa upendo ‘tunapoleta habari njema za jambo bora.’—Isa. 52:7; Mdo. 5:42.