Watasikiaje?
1. Kwa nini kazi ya kuhubiri si rahisi nyakati nyingine, na kwa nini tunaendelea kuhubiri?
1 Kwa sababu siku ya Yehova inakaribia haraka, kuna uhitaji wa haraka wa kuwasaidia watu wengi zaidi wapate ujuzi sahihi wa Mungu na kusudi lake kwa wanadamu. (Yoh. 17:3; 2 Pet. 3:9, 10) Nyakati nyingine si rahisi kufanya hivyo, kwa kuwa watu wengi hawapendezwi au wanatudhihaki kwa sababu ya kazi yetu ya kuhubiri. (2 Pet. 3:3, 4) Hata hivyo, tuna kila sababu ya kuamini kwamba bado kuna watu fulani katika eneo letu ambao watakubali habari njema wanapoisikia. Watu kama hao watasikiaje bila mtu wa kuhubiri?—Rom. 10:14, 15.
2. Mfano wa Paulo unatutia moyo jinsi gani?
2 Kukabiliana na Upinzani: Kwa kuwa bado kuna watu wengi ambao wako tayari kusikiliza ujumbe wa Ufalme, hatupaswi kuvunjika moyo. Filipi lilikuwa jiji la kwanza huko Ulaya kusikia habari njema kutoka kwa mtume Paulo. Baada ya kushtakiwa kwa uwongo, yeye na Sila walipigwa kwa fimbo na kutupwa gerezani. (Mdo. 16:16-24) Hata hivyo, mambo hayo yenye kuumiza hayakumfanya Paulo aogope na kuacha kuhubiri. Alipotembelea Thesalonike, jiji lililofuata katika safari yake ya umishonari, ‘alijipa ujasiri kwa njia ya Mungu.’ (1 The. 2:2) Bila shaka, mfano wa Paulo unaonyesha sababu ya ‘kutokufa moyo.’—Gal. 6:9.
3. Ni nini kinachoweza kufanya watu fulani ambao hawakupendezwa wabadili mtazamo wao?
3 Watu wengi ambao wamekataa kutusikiliza kwa miaka mingi wamebadili mtazamo wao kuhusu ujumbe wetu. Mabadiliko ya kiuchumi, ugonjwa, kifo cha mtu fulani katika familia, habari kuhusu matukio yenye kuhuzunisha ulimwenguni, zinaweza kumfanya mtu abadili mtazamo wake. (1 Kor. 7:31) Wengine ambao wazazi wao walipinga wamekuwa watu wazima na wako tayari kusikiliza. Tunapoendelea kuhubiri tunawapa watu kama hao nafasi ya ‘kuliitia jina la Yehova’ kabla ya wakati kwisha.—Rom. 10:13.
4. Ni nini kinachotuchochea tuendelee katika huduma “bila kuacha”?
4 “Bila Kuacha”: Upendo wetu kwa Mungu na kwa jirani utatuchochea tuendelee kuhubiri na kufanya wanafunzi “bila kuacha,” kama mitume walivyofanya katika karne ya kwanza. (Mdo. 5:42) Leo, kuna watu wengi “wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo yote” yanayofanywa sasa. (Eze. 9:4) Watu hao hupata tumaini na kitulizo kilichoje wanaposikia habari njema! Hata kama wengi hawatasikiliza, tuna uhakikisho wa Kimaandiko kwamba Yehova anapendezwa vema na jitihada zetu.—Ebr. 13:15, 16.