Tunapindua Ngome Zenye Nguvu
1 Kwa karne nyingi, Shetani ameweka vizuizi katika mioyo na akili za watu wengi kwa kutumia mafundisho ya uwongo na udanganyifu. Ameendeleza mafundisho kama vile Utatu, kutokufa kwa nafsi, na moto wa mateso. Anawafanya watu watilie shaka kuwapo kwa Muumba na ikiwa kweli Biblia ilitoka kwa Mungu. Ubaguzi na utaifa ni vizuizi vingine vikubwa vinavyowazuia watu wasiikubali kweli. (2 Kor. 4:4) Tunaweza kufanya nini ili kupindua imani hizo zilizo kama ngome zenye nguvu?—2 Kor. 10:4, 5.
2 Hisia Zinahusika: Mara nyingi mafundisho ya kidini ambayo watu wameamini kwa muda mrefu yanahusisha hisia za ndani sana. Watu fulani wameamini mafundisho ya uwongo tangu walipokuwa watoto. Ili kuwasaidia, tunahitaji kuzungumza kwa njia inayoonyesha kwamba tunaheshimu maoni yao.—1 Pet. 3:15.
3 Tunaweza kuonyesha kwamba tunawaheshimu watu hao kwa kuwaruhusu waeleze mambo wanayoamini na kwa nini wanayaamini. (Yak. 1:19) Huenda wanaamini kwamba nafsi haiwezi kufa kwa sababu wamefiwa na wanatamani sana kuwaona tena watu wao waliokufa. Au huenda wakaadhimisha sikukuu kwa sababu wanaona hizo ni pindi za kuwa pamoja na watu wa familia yao. Kusikiliza maoni yao kutatusaidia kufahamu hisia zao na kutoa jibu linalofaa.—Met. 16:23.
4 Mwige Yesu: Yesu alituwekea mfano bora alipojibu maswali ya mtu aliyeijua sana Sheria. Yesu hakutoa majibu ya moja kwa moja, kwa kuwa mtu huyo angeyakataa kwa sababu alipenda sana mambo aliyoyaamini. Badala yake, Yesu alimwelekeza kwenye Maandiko, akamwomba aeleze maoni yake, naye akatumia mfano ili kumsaidia kufikiri.—Luka 10:25-37.
5 Kweli ya Neno la Mungu ina nguvu za kupindua mafundisho ya uwongo ya kidini ambayo watu wameyashikilia sana. (Ebr. 4:12) Tukijitahidi kuwafikia moyo kwa subira, huenda tukawasaidia kukataa uwongo na kuikubali kweli ambayo inaweza kuwaweka huru.—Yoh. 8:32.