Kujitayarisha—Siri ya Kufanya Ziara za Kurudia Zenye Manufaa
1. Huduma ya Wakristo wa mapema ingeongezekaje?
1 Yesu aliwatayarisha kabisa wanafunzi wake ili wawe wahubiri stadi wa “habari njema ya ufalme.” (Mt. 4:23; 9:35) Aliwazoeza alipokuwa akihubiri katika Palestina. Hata hivyo, kabla ya kupanda kwenda mbinguni, Yesu alitangaza kwamba huduma ya Kikristo ingeongezeka sana ili ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’—Mt. 28:19, 20.
2. Ni nini kinachohusika katika kutii amri ya Yesu ya ‘kufanya wanafunzi’?
2 Kazi hiyo ingehusisha kuwarudia watu wanaopendezwa na habari njema ya Ufalme wa Mungu na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo Kristo aliamuru. Ili kufanya ziara za kurudia zenye manufaa, tunahitaji kujitayarisha vizuri.
3. Hata katika ziara ya kwanza, unaweza kufanya nini ili uweke msingi wa ziara ya kurudia?
3 Panga Mapema: Wahubiri fulani wanajitahidi kuuliza swali mwishoni mwa ziara ya kwanza na kuahidi kurudi kuzungumzia jibu. Wamegundua kwamba kutaja habari iliyo katika kitabu Biblia Inafundisha kwenye ziara ya kurudia, kumewasaidia kuanzisha funzo la Biblia moja kwa moja.
4. Kwa nini hatupaswi kukawia kufanya ziara ya kurudia eti kwa sababu tunangojea magazeti mapya?
4 Ikiwa tuna magazeti ya mwezi mmoja tu, si lazima tungoje hadi tupokee magazeti ya mwezi unaofuata ili turudi. Tunaweza kumchochea mtu huyo aendelee kupendezwa kwa kuzungumzia habari zilizo katika gazeti ambalo tayari analo.
5. Kuna faida gani kuwa na lengo akilini?
5 Uwe na Lengo: Kabla ya kurudi, tenga dakika chache kupitia rekodi zako na kuamua mambo unayotaka kutimiza. Kwa mfano, unaweza kuzungumzia jambo fulani katika kitabu ulichokuwa umeacha. Au unaweza kuacha kichapo kingine kinachohusiana na jambo fulani ambalo mlizungumzia. Ikiwa uliuliza swali katika ziara iliyopita, lengo lako litakuwa kujibu swali hilo. Unapozungumzia andiko linalokazia hoja fulani, lisome moja kwa moja katika Biblia.
6. Lengo letu ni nini tunapofanya ziara za kurudia?
6 Lengo Letu: Bila shaka, lengo letu ni kuanzisha funzo la Biblia. Ndugu mmoja alitaka kuanzisha funzo la Biblia pamoja na mtu fulani kwenye ziara ya kurudia, lakini mtu huyo akakataa. Ndugu huyo alirudi akiwa na magazeti ya karibuni na kusema, “Leo, tunajibu swali moja la Biblia ambalo watu wanauliza.” Baada ya kupata maelezo ya mtu huyo, ndugu huyo alisoma andiko na fungu lililohusiana nalo katika kitabu kinachotumiwa kuongoza mafunzo ya Biblia. Funzo la Biblia likaanzishwa, nalo likaendelea kwa ukawaida.
7. Kujitayarisha vizuri kumekusaidiaje kuanzisha funzo la Biblia?
7 Kuna faida za kujitayarisha kwa ajili ya ziara za kurudia. Shangwe yetu itaongezeka, na huenda tukapata pendeleo la kumsaidia mtu aliye na “mwelekeo unaofaa” aanze kutembea katika barabara inayoenda kwenye uzima.—Mdo. 13:48.