Tuna Hazina za Kuwagawia Wengine
1 Neno la Mungu lina mafundisho mengi yenye manufaa ambayo tunayathamini. (Zab 12:6; 119:11, 14) Pindi moja, Yesu alitumia mifano kufafanua mambo mbalimbali kuhusu Ufalme, kisha akawauliza wanafunzi wake hivi: “Je, mlipata maana ya mambo yote haya?” Waliposema wamepata maana, akawaambia: “Ikiwa ni hivyo, kila mfundishaji wa watu wote, anapofundishwa kuhusiana na ufalme wa mbinguni, ni kama mtu, mwenye nyumba, ambaye hutoa katika hazina yake vitu vipya na vya zamani.”—Mt. 13:1-52.
2 Kweli za Biblia tulizofundishwa tulipoanza kujifunza ni kama hazina za zamani. Tunapoendelea kujifunza Neno la Mungu kwa undani, tunapata kujua kweli nyingine pia, ambazo tunaziona kuwa hazina mpya. (1 Kor. 2:7) Pia, kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” tunajifunza kweli mpya.—Mt. 24:45.
3 Tunathamini sana hazina hizi za kiroho, ziwe za zamani au ziwe mpya. Jambo hilo hutuchochea tujitahidi kupata mazoezi katika kuwafundisha watu Neno la Mungu, huku tukiwaeleza kwa shauku kweli zenye thamani ambazo tumejifunza.
4 Jifunze Kutoka kwa Yesu: Yesu alionyesha jinsi alivyohisi kuhusu hazina hizi kwa kujitahidi sana kuwaeleza wengine kuzihusu hata alipokuwa amechoka.—Yoh. 4:6-14.
5 Upendo wa Yesu kwa wale ambao hawakujua ukweli kumhusu Mungu na kusudi lake, ulimsukuma awaeleze kweli za Mungu ambazo ni hazina inayowapa watu uhai. (Zab. 72:13) Aliwasikitikia wale waliokuwa na njaa ya kiroho na akasukumwa “kuwafundisha mambo mengi.”—Marko 6:34.
6 Mwige Yesu: Tunapothamini hazina tulizo nazo, tutakuwa na tamaa kama Yesu ya kuwaonyesha watu hazina hizo moja kwa moja katika Biblia. (Met. 2:1-5) Ijapokuwa huenda nyakati nyingine tukawa tumechoka, tutazungumza kuhusu kweli za Biblia kwa shauku nyingi. (Marko 6:34) Uthamini wetu mwingi kwa hazina hizi utatuchochea tufanye yote tuwezayo, yaani, nyakati zote tutajitahidi kushiriki kwa kadiri kubwa zaidi katika huduma.