Wafundishe Watu Wasioweza Kusoma Vizuri
1. Huenda tukakabili tatizo gani katika huduma?
1 Tunaposhiriki katika huduma, mara kwa mara tunakabili tatizo la kuwafundisha kweli watu wasioweza kusoma vizuri. Tunaweza kufanya nini?
2. Tunawaonyesha heshima watu wasioweza kusoma vizuri katika njia gani, na kwa nini tunafanya hivyo?
2 Waonyeshe Heshima: Yehova anapendezwa na hali ya moyoni ya mtu, bali si kiwango chake cha elimu. (1 Sam. 16:7; Met. 21:2) Kwa hiyo, hatuwadharau watu wasioweza kusoma vizuri. Itakuwa rahisi zaidi kwa watu kama hao kukubali msaada wetu tukiwaonyesha heshima na subira. (1 Pet. 3:15) Tunaweza kufanya hivyo kwa kutosisitiza kwamba mtu asome andiko au fungu. Mtu anapoendelea kujifunza kweli zenye thamani za Biblia, huenda akawa na hamu zaidi ya kuboresha usomaji wake ili apate shangwe ya kusoma Neno la Mungu “kwa sauti ya chini mchana na usiku.”—Zab. 1:2, 3.
3. Ni njia gani za kufundisha ambazo zinaweza kutumiwa kuwafundisha wale wasioweza kusoma vizuri?
3 Njia Mbalimbali za Kuwafundisha Wanafunzi wa Biblia: Kutumia picha ni njia bora ya kufundisha na kumsaidia mwanafunzi akumbuke mambo anayojifunza. Unaweza kumuuliza maoni yake kuhusu picha fulani katika kitabu mnachojifunza. Kisha utumie maswali hususa kumsaidia aelewe jambo ambalo picha hiyo inafundisha. Tumia maandiko yanayokazia mambo fulani kuhusu picha hiyo. Picha zinaweza kutumiwa pia kuyapitia mambo makuu mliyojifunza. Msijifunze mambo mengi mno kwa wakati mmoja. Kazia kichwa na mambo makuu katika somo, na uepuke kuzungumzia mambo ya ziada yasiyo katika somo. Soma maandiko moja kwa moja katika Biblia, na utumie maswali kuhakikisha kwamba mwanafunzi anaelewa andiko lililosomwa. Huenda hilo likaongeza hamu yake ya kuboresha uwezo wake wa kusoma ili ajifanyie utafiti zaidi kuhusu kweli za Biblia.
4. Tunaweza kumsaidiaje mwanafunzi aboreshe uwezo wake wa kusoma?
4 Vifaa vya Kumsaidia Mwanafunzi Aboreshe Usomaji Wake: Watu wasioweza kusoma vizuri au ambao hawakupata nafasi ya kujizoeza kusoma kwa ufasaha, wanaweza kuelewa na kushika mambo vizuri sana. Unaweza kuwatia moyo wasikilize vichapo vilivyorekodiwa. Mwanafunzi atasaidiwa kuboresha usomaji wake anapomsikiliza kwa makini msomaji, huku akifuatana naye kwa kusoma nakala yake mwenyewe na hata kutamka kwa sauti ya chini maneno yanayosomwa. Broshua Jitahidi Kusoma na Kuandika inaweza kumsaidia pia. Katika maeneo fulani, wazee wanaweza kupanga kuwe na darasa la kujifunza kusoma katika kutaniko. Kwa kutumia madokezo hayo tunaweza kuwasaidia wale wasioweza kusoma vizuri waelewe “maandishi matakatifu,” yanayoweza kuwafanya wawe wenye hekima kwa ajili ya wokovu.—2 Tim. 3:15.