Huduma Yetu Inaonyesha Kwamba Tunampenda Mungu
1. Yesu alisukumwa kufanya nini kwa sababu alimpenda Mungu?
1 Upendo ulimsukuma Yesu atimize huduma yake. Sehemu zote za huduma ya Yesu zilionyesha waziwazi kwamba anampenda Yehova. Yesu alisema: “Kusudi ulimwengu ujue kwamba ninampenda Baba, kama vile Baba amenipa amri kufanya, ndivyo ninavyofanya.” (Yoh. 14:31) Sisi pia, ambao ni wafuasi wa Yesu, tuna pendeleo la kuonyesha katika huduma yetu kwamba tunampenda Mungu kwa moyo wote.—Mt. 22:37; Efe. 5:1, 2.
2. Upendo wetu kwa Yehova unatusukuma kufanya nini katika huduma?
2 “Jina Lako na Litakaswe”: Tunapotumia kila fursa tunayopata kuzungumza na wengine kumhusu Yehova na Ufalme wake, tunaonyesha kwamba tunampenda Mungu, na hivyo tunachangia kutakaswa kwa jina lake. (Zab. 83:18; Eze. 36:23; Mt. 6:9) Kwa kuendelea na huduma yetu tunaonyesha kwamba tunatamani kwa moyo wote, kama Yesu alivyotamani, kuona jina la Yehova likitakaswa na mapenzi yake yakitendeka.—Mt. 26:39.
3. Upendo wetu kwa Yehova unatusaidiaje kushinda vikwazo?
3 Upendo Unatuchochea Tushinde Vikwazo: Upendo kwa Yehova unashinda vikwazo vyote. (1 Kor. 13:4, 7) Yesu alikabili hali mbalimbali maishani mwake ambazo zingaliweza kumzuia asiendelee na huduma yake. Hata hivyo, aliweza kushinda vikwazo vyote alivyovikabili kwa sababu alimpenda Yehova kwa moyo wote na alitaka kufanya mapenzi yake. (Marko 3:21; 1 Pet. 2:18-23) Sisi pia tunakabili matatizo mengi ambayo upendo wetu kwa Mungu unaweza kutusaidia kuyashinda. Kwa kufuata kwa makini mfano wa Kristo, tunaweza kuwa wenye hakika tunapoendelea kufanya yote tuwezayo katika huduma yetu. Ijapokuwa tunaathiriwa na upinzani wa watu wa familia, afya mbaya, uzee, au ubaridi wa watu wasiopendezwa, bado tunaendelea kuonyesha kwamba tunampenda Yehova kwa kutimiza huduma yetu kikamili iwezekanavyo.
4. Tuna pendeleo gani kwa sababu tunampenda Yehova?
4 Upendo una nguvu sana, na katika huduma yetu tunaweza kuonyesha kwamba tunampenda Mungu kwa moyo wote. (1 Kor. 13:13) Tunapokaribia haraka wakati ambapo jina la Yehova litatakaswa daima dawamu, ‘upendo wetu na uwe mwingi hata zaidi na zaidi.’—Flp. 1:9; Mt. 22:36-38.