Je, Ninatimiza Huduma Yangu vya Kutosha?
1. Ni mambo gani ambayo huenda yakamhangaisha Mkristo mwaminifu?
1 Je, umewahi kujiuliza swali hilo? Huenda ukavunjika moyo kwa kuwa hushiriki sana katika huduma kama ulivyokuwa ukishiriki hapo awali kwa sababu ya umri, matatizo ya kiafya, au kuongezeka kwa majukumu ya familia. Dada mmoja aliye na watoto watatu aliandika kuwa wakati mwingine yeye huhisi vibaya, kwa sababu wakati na nguvu anazotumia kutunza familia yake humfanya asitimize mengi katika huduma. Ni nini kitakachotusaidia kuona mambo kwa njia yenye usawaziko?
2. Yehova anatazamia nini kutoka kwetu?
2 Yehova Anatazamia Nini Kutoka Kwetu?: Bila shaka, sisi sote tungependa kufanya mengi zaidi katika huduma. Lakini kuna tofauti kubwa kati ya mambo ambayo tungependa kufanya na mambo ambayo tunaweza kufanya. Kwa kuwa tunatamani kufanya mengi zaidi, ni wazi kuwa tunahisi kutoridhika na yale tunayofanya. Tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova anajua vizuri kile tunachoweza kutimiza na hadai mengi kuliko uwezo wetu. (Zab. 103:13, 14) Yeye anatazamia nini kutoka kwetu? Anataka tumtumikie kwa moyo wote, na tumtolee utumishi bora.—Kol. 3:23.
3. Tunawezaje kutambua uwezo wetu katika huduma?
3 Ni nini kitakachoweza kutusaidia kutambua uwezo wetu kihalisi? Tunaweza kusali kwa Yehova atusaidie kuona hali yetu kihalisi. (Zab. 26:2) Mkristo mkomavu tunayemwamini, anayetujua vizuri, na asiyeogopa kutuambia mambo tunayohitaji kuboresha, anaweza kutusaidia pia. (Met. 27:9) Usisahau kuwa hali hubadilika, hivyo, inafaa kujichunguza mara kwa mara.—Efe. 5:10.
4. Tunapaswa kuvionaje vikumbusho kuhusu huduma?
4 Tuvioneje Vikumbusho Kuhusu Huduma?: Wakati wa shindano la mbio, watazamaji huwatia moyo wakimbiaji kwa kuwashangilia. Kusudi kuu huwa kuwasaidia wakimbiaji wafikie lengo lao na si kuwavunja moyo. Vivyo hivyo, kitia moyo kinachotegemea Biblia na vikumbusho vya ‘kuhubiri neno kwa bidii,’ tunavyopata mikutanoni na katika vitabu vyetu ni kwa faida yetu wenyewe na si vya kutuonyesha kuwa jitihada zetu ni za bure. (2 Tim. 4:2) Tunaweza kuwa na uhakika kuwa, ikiwa tutaendelea kujaribu kufanya yote tuwezayo, Yehova atakumbuka na kutubariki kwa ajili ya ‘upendo na kazi zetu.’—Ebr. 6:10.