Kampeni Ambayo Huwa na Matokeo Mazuri
Majuma matatu kabla ya kusanyiko kuanza, kwa mara nyingine tena makutaniko yatapata fursa ya kushiriki katika kampeni ya kuwaalika wale wanaopendezwa wahudhurie kusanyiko. Kuna sababu nzuri ya kufanya kampeni hiyo ya kila mwaka. Kwa kawaida, wale wanaopokea mialiko na kuhudhuria kusanyiko huvutiwa sana na hotuba za Kimaandiko, idara zenye mpangilio mzuri zinazoshughulikiwa na watu waliojitolea, na mwenendo mzuri na umoja tunaoonyesha. (Zab. 110:3; 133:1; Isa. 65:13, 14) Ingawa hivyo, je, watu hukubali mialiko na kuhudhuria kusanyiko? Vipi katika maeneo ambayo wale wanaopendezwa hulazimika kusafiri mbali ili kuhudhuria kusanyiko?
Baada ya kusanyiko la wilaya la mwaka wa 2011, ofisi moja ya tawi ilipokea barua kutoka kwa mwanamke aliyepata mwaliko kwenye mlango wake. Kila mara Mashahidi wa Yehova walipogonga mlango wake alijificha. Aliandika hivi: “Nilikuwa na nyumba nzuri, mume mzuri, na nilifikiri nilikuwa na kila kitu nilichohitaji ili niwe na furaha. Kwa kusikitisha, bado sikuwa na furaha, na maisha yangu kwa kweli hayakuwa na kusudi. Kwa hiyo niliamua kuendesha gari umbali wa kilometa 320 ili kuhudhuria programu ya siku ya Jumamosi.” Alifurahia sana kusanyiko hivi kwamba alimpigia simu mume wake na kumweleza kwamba hangerudi nyumbani usiku huo ili ahudhurie pia siku ya Jumapili. “Nilisikiliza hotuba zote, nilikutana na Mashahidi wengi wa Yehova, nami sikutaka kuachia hapo.” Baada ya kurudi nyumbani, alianza kujifunza na baada ya miezi minne akawa mhubiri ambaye hajabatizwa. “Ninafurahi sana kwamba nilipata mwaliko huo kwenye mlango wangu kwa sababu sasa maisha yangu yana kusudi kweli kweli!”
Baadhi ya wale wanaopokea mwaliko watahudhuria. Hivyo, shiriki kwa bidii katika kampeni hiyo muhimu. Beba mialiko yoyote iliyobaki unapoenda kwenye mji ambao kusanyiko litafanywa, na uitumie kuhubiri isivyo rasmi.
[Sanduku katika ukurasa wa 4]
Tutatoaje Mialiko?
Ili tuwafikie wote katika eneo letu, tunapaswa kuzungumza kwa ufupi. Tunaweza kusema: “Habari. Tunashiriki katika kampeni ya ulimwenguni pote ya kusambaza mwaliko huu. Huu ni mwaliko wako. Utapata habari zaidi katika mwaliko huu.” Uwe mchangamfu. Inapofaa, tunapaswa pia kutoa magazeti tunaposhiriki katika kampeni hiyo Jumamosi na Jumapili.