Mwaliko wa Pekee
1. Kampeni ya kuwaalika watu kwenye makusanyiko ya mwaka 2014 itaanza lini?
1 Ikiwa unatayarisha mlo maalumu kwa ajili ya familia na marafiki, na umetumia jitihada na gharama nyingi, bila shaka utawakaribisha wageni wako kwa shauku. Vivyo hivyo, kazi nyingi imefanywa kuandaa karamu ya kiroho kwenye makusanyiko yetu ya eneo na ya kimataifa ya mwaka 2014. Majuma matatu kabla ya kusanyiko letu, tutakuwa na pendeleo la kuwaalika wengine wahudhurie. Ni nini kitakachotusaidia kuwaalika watu kwa shauku?
2. Ni nini kitakachokuchochea kushiriki katika kampeni kwa bidii?
2 Tukithamini jinsi tunavyofaidika kibinafsi kutokana na karamu ambayo Yehova anatuandalia kwenye makusanyiko yetu, tutachochewa kushiriki kampeni hiyo kwa bidii. (Isa. 65:13, 14) Tunapaswa kukumbuka kwamba kampeni hiyo ya kila mwaka huwa na matokeo mazuri. Baadhi ya wale ambao tutawakaribisha watahudhuria. Hata kama watakaohudhuria watakuwa wachache, jitihada zetu wakati wa kampeni zitamletea Yehova sifa na kuonyesha jinsi alivyo mkarimu.—Zab. 145:3, 7; Ufu. 22:17.
3. Mialiko itasambazwaje?
3 Mabaraza yote ya wazee yanapaswa kuamua jinsi makutaniko yao yatakavyosambaza mialiko kwa watu wengi iwezekanavyo, kutia ndani iwapo wataacha mialiko hiyo wanapowakosa wenye nyumba au wataitoa wanapohubiri hadharani. Katika mwisho-juma, iwapo inafaa, tunapaswa kutoa magazeti pamoja na mialiko. Ikiwa Jumamosi ya kwanza ya mwezi imeangukia kwenye tarehe za kampeni, tunapaswa kuzingatia zaidi kazi ya kugawa mialiko badala ya kuanzisha mafunzo ya Biblia. Mwishoni mwa kampeni tutafurahi sana kujua kwamba tulishiriki kwa bidii na shauku kuwaalika watu wengi iwezekanavyo wajiunge nasi katika karamu ya kiroho ambayo Yehova ametuandalia!